Monday, August 21, 2017

CHAMA CHA ADC CHASHEREHEKEA KUTIMIZA MIAKA MITANO TANGU KUANZISHWA KWAKE


Siku ya jana Chama Cha Alliance for Democratic Change (ADC) chenye kaulimbiu ya Dira ya Mabadiliko kimetimiza miaka mitano tangu kupata usajili rasmi 22 Agosti 2012.
Akizungumza katika maadhimisho ya Chama hicho Mwenyekiti wa chama hicho Hamad Rashid ambaye pia ni Waziri wa Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi Zanzibar, ametoa wito kwa vyama vya siasa kuiga mfano wa ADC ambao wamekuwa wakimaliza migogoro yao kwa njia ya mazungumzo kwa kipindi hicho cha miaka mitano tofauti na vifanyavyo vyama vingine.

Mwenyekiti Hamad Rashid ameuzungumzia mgogoro unaoendelea ndani ya Chama cha CUF na kueleza kuwa hatua waliyofikia ya kupelekana mahakami siyo sahihi kwani itazidi kuchochea mgogoro huo.
"Mahakama kazi yake ni kuhukumu mmoja lazima akose na mwingine lazima apate kutokana na hukumu, ni vyema viongozi wawili wanaoonekana kutajwa katika mgogoro huo Profesa Lipumba na Maalim Seif kukaa katika meza moja ya majadiliano na kuutatua mgogoro huo" Alisema Hamad Rashid.

Hamad Rashid amefafanua kuwa ADC ilikuwa na mgogoro na aliyekuwa mwenyekiti wa kwanza wa Chama hicho Said Miraji na wenzake wanne lakini wameumaliza mgogoro wao kwa majadiliano bila kufikishana mahakamani, hivyo ni vyema CUF wakaiga mfano huo na kuziondoa tofauti zao.

Naye Katibu Mkuu wa Chama hicho Doyo Hassan Doyo ameeleza kuwa zuio la kufanya mikutano ya kisiasa limekwamisha utendaji kazi wa ADC kama chama kinachohitaji kujitangaza kwa wananchi.

Vilevile Katibu Mkuu Doyo amesisitiza kuwa Chama chao kitaendelea kupinga vikali kuwatumia vijana katika kufanya vurugu na maandamano yasiyo na tija, ndoa za jinsia moja, na adhabu ya kifo.

No comments: