Monday, March 27, 2017

WAKULIMA WA ALIZETI MKOANI SINGIDA WAAZIMIA KUTEKA SOKO LA ZAO HILO NCHINI




Afisa kilimo na Mratibu wa MIVARF Mkoa wa Singida akimsikiliza mkulima wa Alizeti Mkoa wa Singida akipalilia zao hilo, mkulima huyu amefuata ushauri wa kitaalamu wa kupanda kwa mistari, kuweka mbolea na kutumia mbegu mpya ya record ambayo huzalisha kwa wingi.
Mkulima wa Alizeti Mkoa wa Singida akipalilia zao hilo, mkulima huyu amefuata ushauri wa kitaalamu wa kupanda kwa mistari, kuweka mbolea na kutumia mbegu mpya ya record ambayo huzalisha kwa wingi.


Wakulima wa alizeti Mkoani Singida wameazimia kuwa wazalishaji namba moja nchini wa alizeti kwa wingi na ubora wa hali ya juu kutokana na kutumia mbinu bora na za kisasa huku wakiachana na kilimo cha mazoea kilichowapa matokeo kidogo na yasiyo na ubora.

Wakulima wa Wilaya tatu za Iramba, Manyoni na Singida wamefikia uamuzi huo katika vikao kati yao na kamati ya ufuatiliaji wa progamu ya Uboreshaji wa Miundombinu ya Masoko, Uongezaji wa thamani ya mazao na Huduma za kifedha vijijini (MIVARF) iliyokuwa ikifanya tahmini ya mradi huo kwa kutembelea mashamba na kuzungumza na wakulima hao.

Mwenyekiti wa Kikundi cha Mwangaza cha wakulima wa Alizeti kata ya Sanjaranda Wilayani Manyoni Bi. Janeth Emmanuel amesema, mradi wa MIVARF umewahamasisha kutumia mbegu ya alizeti ya kisasa aina ya record ambayo huzalisha wastani wa gunia 12 mpaka 16 kwa ekari moja wakati mbegu ya zamani ambayo walikuwa wakiitumia ya zebra imekuwa ikizalisha gunia mbili mpaka nne kwa ekari moja.

Bi Janeth amesema kutokana na wakulima wengi kuhamasika kutumia mbegu mpya ya record na kufuata elimu waliyopewa na MIVARF, Mkoa wa Singida utazalisha alizeti nyingi na bora kwa ajili ya viwanda vya ndani na nje ya Mkoa.

Amesema wakulima wa alizeti walikua hawafuati ushauri wa kupanda zao hilo kwa mistari, kuacha nafasi pamoja na kuweka mbolea ambapo awali walidhani alizeti haihitaji kuwekewa mbolea kitu ambacho sio sahihi na hivyo kupelekea mkulima kutumia eneo kubwa na kuzalisha kidogo.

Bi. Janeth ameongeza kuwa kutokana na matarajio ya kuvuna alizeti nyingi elimu zaidi juu ya uongezaji wa thamani wa alizeti itolewe kwa wakulima ili waweze kupata faida kubwa tofauti na awali ambapo wamekuwa wakimwaga mashudu ambayo huzalisha kiwi na mkaa na kuuza alizeti ghafi badala ya mafuta.

Naye Mtoa huduma wa MIVARF Wilaya ya Manyoni Anthony Mtu amesema mradi huo umewafikia wakulima elfu mbili katika kata ya Sanjarada huku wakianzisha mashamba darasa 12 ya zao la alizeti yenye ukubwa wa ekari 24 huku matarajio ya mavuno kwa mashamba darasa yakiwa ni magunia 288.

Mtu amesema wakulima wamehamasika kutumia mbegu ya record baada ya kuelimishwa kuwa mbegu hiyo, inatumia maji kwa ufanisi, inatoa mavuno mengi na haishambuliwi na magonjwa kwa urahisi.

Kwa upande wake Afisa Kilimo na Mratibu wa MIVARF Mkoa wa Singida Lucas Mkuki amesema mradi huo umeanza kutekelezwa mwaka 2011 ukiwa unafadhiliwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika.

Mkuki amesema katika wilaya zote Mradi umeweza kukarabati barabara ili kurahisisha wakulima kusafirisha alizeti ambapo barabara zilizokarabatiwa ni ya Muhanga-Mwakajenga wilaya ya Manyoni kilometa 20, Njiapanda-Ngimu Wilayani Singida Kilometa 28 na wilayani Iramba kilometa 1.4 ujenzi wake utaanza hivi karibuni.

Ameongeza kuwa mradi umefanikisha ujenzi wa maghala yenye uwezo wa kuhifadhi mazao kiasi cha tani 1000 katika kijiji cha Mtinko wilayani Singida, kijiji cha Nselembwe wilayani Manyoni na kijiji cha Sanjaranda wilayani Manyoni.

Mkuki amesema mradi wa MIVARF umewajengea uwezo wazalishaji wa alizeti kuyafikia masoko na kuongeza thamani ya zao hilo huku akiwasisitiza wakulima kuendeleza elimu na vikundi vilivyozalishwa na mradi huo endapo mradi utafikia ukomo wa utekelezaji wake.

No comments: