Saturday, January 21, 2017

WANANCHI WATAKIWA KUJITOKEZA KWA WINGI KUPIGA KURA UCHAGUZI MDOGO WA UDIWANI NA UBUNGE.

Na Aron Msigwa –NEC, Zanzibar.

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imewataka wananchi wanaoishi katika kata 19 zitakazofanya Uchaguzi mdogo wa Madiwani  kwa upande  Tanzania Bara na Ubunge katika jimbo la Dimani Zanzibar Januari 22, 2017 wajitokeze kwa wingi kupiga kura kuwachagua viongozi watakaowaongoza kwa kipindi cha miaka 3. 
Akizungumza na vyombo vya Habari leo mjini Zanzibar, Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Jaji wa Rufaa, Mhe. Semistocles kaijage amesema kuwa maadalizi ya Uchaguzi huo yamekamilika na wananchi wenye sifa za kupiga kura katika uchaguzi huo wajitokeze kutimiza wajibu wao wa Kikatiba. 
Mhe. Kaijage amewapongeza wananchi wanaoishi katika Jimbo la Dimani,  Zanzibar na wale wa Kata 19 za Tanzania Bara zitakazofanya uchaguzi mdogo hapo kesho  kwa utulivu waliouonyesha wakati wa kipindi cha Kampeni za Uchaguzi huo. 
 Ameeleza kuwa licha ya kuwepo kwa dosari za hapa na pale zilizojitokeza zikiwemo za ukiukwaji wa Maadili ya Uchaguzi kwa baadhi ya Vyama na wagombea wao, Tume ya Taifa ya Uchaguzi ilichukua hatua za kukemea vitendo hivyo ili kuwezesha Kampeni za Uchaguzi kufanyika kwa Usalama na Amani. 
“Licha ya kwamba kutakuwa na ulinzi wa kutosha katika vituo vya kupigia kura, Ni matumaini ya Tume kuwa hali ya Amani na Utulivu ambayo imekuwepo hadi sasa na kama ilivyokuwa katika Chaguzi zilizopita itaendelea kudumishwa ili kuhakikisha uchaguzi huu unafanyika kwa Utulivu, Amani na Ustawi wa Taifa letu” Amesema Jaji Kaijage. 
Ameeleza kuwa katika uchaguzi huo  jumla ya Wapiga Kura 9,280 wa Jimbo la Dimani Zanzibar wanatarajiwa kupiga kura ili kumchagua Mbunge atakayewaongoza kwa kipindi cha miaka 3 kupitia vituo 29 vya Kupigia Kura katika Jimbo hilo. 
Kwa upande wa Uchaguzi Mdogo wa Madiwani katika Kata 19 za Tanzania Bara Wapiga Kura 134,705 walioandikishwa wanatarajia kupiga kura  katika vituo 359 ambavyo vilitumika katika Uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.
Naomba nitumie fursa hii kutoa rai kwa wananchi waliojiandikisha wajitokeze kwenye vituo vilivyotumika wakati wa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 ili waweze kupiga kura kuwachagua viongozi mnaowataka bila hofu, woga, wasiwasi au ushawishi” Amesisitiza. 
Kuhusu mchakato mzima upigaji wa kura ikiwemo taratibu za kuzingatiwa na wananchi kwenye vituo vya kupigia Kura, uhesabuji wa Kura, ujumlishaji wa Kura na Utangazaji wa matokeo amesema kuwa hatua zote zitafanywa na Wasimamizi wa Uchaguzi kwa kuzingatia Sheria. 
Amesema kuwa siku ya uchaguzi Januari 22, 2017 vituo vyote  vitafunguliwa saa 1:00 asubuhi na kufungwa saa 10:00 jioni na kufafanua kuwa iwapo wakati wa kufunga Kituo watakuwepo Wapiga Kura katika mstari ambao wamefika kabla ya saa kumi jioni na hawajapiga wataruhusiwa Kupiga Kura. 
Jaji Semistocles amesisitiza kwamba mtu yeyote hataruhusiwa kujiunga katika mstari wa Wapiga Kura baada ya saa kumi (10:00) jioni  muda ulioainishwa kisheria.
Ameeleza kuwa kwa kila mpiga kura katika jimbo hilo akumbuke kubeba Kadi yake ya Mpiga Kura kwa kuwa Sheria ya Uchaguzi inaelekeza kuwa ili Mpiga Kura aruhusiwe kupiga kura ni lazima awe na kadi ya Mpiga Kura. 
“ Naomba ieleweke wazi kuwa Fomu Na. 17 sio mbadala wa Kadi ya Mpiga Kura, Wapiga Kura ambao wana Kadi ya Mpiga Kura lakini taarifa zao hazimo katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura Kituoni, hawataruhusiwa kupiga kura” Amesisitiza Jaji Kaijage.
Amesema kuwa ni  marufuku na ni kosa la jinai kumkataza mtu kwenda Kupiga Kura akisisitiza kwamba siku hiyo ya kupiga kura kipaumbele kitatolewa kwa wagonjwa, watu wenye ulemavu, wanawake wajawazito au wenye watoto wachanga na wazee ambao hawatatakiwa kupanga mstari. 
Jaji Semistocles amefafanua kuwa wakati wote wa Kupiga Kura na Kuhesabu Kura, Mawakala wa Vyama vya Siasa watakuwepo kwenye vituo kwa kuwa wajibu wao ni kulinda maslahi ya Vyama vyao vya Siasa na Wagombea wao.
 Hata hivyo amesema hawatakiwi kuingilia masuala ya utendaji ambayo yamekabidhiwa kwa Msimamizi wa Kituo. 
Amesema Mawakala hao wataruhusiwa kuwepo Vituoni kwa mujibu wa Sheria na Kanuni na kusisitiza kwamba Wakala asiyekuwa na barua ya utambulisho kutoka kwa Msimamizi wa Uchaguzi na ambaye hatakula kiapo cha kutunza siri hataruhusiwa kuingia katika Kituo cha Kupigia, Kuhesabia na Kujumlishia Kura. 
Katika hatua nyingine Jaji Kaijage amebainisha kuwa Kura zilizopigwa  zitahesabiwa katika Kituo cha Kupigia Kura mara tu Upigaji Kura utakapokamilika  na matokeo husika ya  Kituo kujazwa kwenye Fomu za Matokeo Na. 21B kwa upande wa  Ubunge na Fomu Na. 21C kwa upande wa  Udiwani kisha fomu hizo kutiwa saini na Msimamizi wa Kituo/Msimamizi Msaidizi wa Kituo, Mawakala wa Vyama au Mgombea aliye Kituoni.  
Amesema nakala moja watapewa Mawakala/Mgombea na nakala nyingine itabandikwa nje ya Kituo cha Kuhesabia kura ambapo Wakala wa kila Chama cha Siasa na mlinzi wa Kituo watakaokuwa Kituoni wataruhusiwa kusindikiza msafara wa kupeleka matokeo ya Uchaguzi kwenda kwa Msimamizi wa Uchaguzi/Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi wa Kata kwa upande wa Tanzania Bara na kwa Msimamizi wa Uchaguzi/Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Dimani kwa upande wa Zanzibar. 
Amefafanua kuwa matokeo yote yakishapokelewa na Msimamizi wa Uchaguzi kwa upande wa Uchaguzi wa Ubunge na Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi kwa upande wa Uchaguzi wa Udiwani, yatajumlishwa mbele ya Mawakala na wote wanaoruhusiwa kuingia kwenye vituo vya Kujumlishia Kura. 
“ Kama ilivyokuwa wakati wa Kuhesabu Kura, baada ya Ujumlishaji kukamilika matokeo ya Ubunge ngazi ya Jimbo yatajazwa katika Fomu Na. 24B na yale ya Diwani katika Kata yatajazwa katika Fomu Na. 24C, Fomu za Matokeo hayo zitatiwa saini na Msimamizi wa Uchaguzi na Mawakala watakaokuwepo watapewa nakala za Fomu za Matokeo na Nakala moja itawekwa mahali pa wazi nje ya Kituo cha Kujumlisha Kura”    
Akitoa ufafanuzi kuhusu kampeni za uchaguzi huo amesema zitamalizika leo (Januari 21)  saa 12 jioni na Vyama, Wagombea na mashabiki hawataruhusiwa kufanya kampeni za aina yoyote ikiwa ni pamoja na kutumia alama zozote zinazoashiria Kampeni kama vile bendera na mavazi ya vyama vyao. 
Kuhusu uwazi katika uendeshaji wa uchaguzi huo amefafanua kuwa vyama vyote vya Siasa vinavyoshiriki katika Uchaguzi   vinatakiwa kuhakikisha kwamba vinaweka Mawakala katika vituo vyote vya Kupigia Kura na Kujumlishia Kura ambao watatimiza majukumu yao kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu zilizowekwa. 
Jaji Kaijage amesisitiza kuwa kwa kuzingatia Maadili ya Uchaguzi ya mwaka 2015 yaliyokubaliwa na Vyama vyote vya Siasa, Wapiga Kura wanatakiwa kuondoka Vituoni mara baada ya kupiga kura ili kuendelea na shughuli zao kwa kuwa  Vyama vya Siasa vyenye wagombea vitakuwa na Mawakala vituoni ambao watalinda maslahi ya Vyama na Wagombea wao huku watu waliotajwa kwenye Sheria ya Uchaguzi wakiwemo wagombea, mawakala, Afisa wa Tume, msimamizi wa Uchaguzi na Afisa Usalama ndiyo wanaoruhusiwa kuingia kwenye Vituo vya Kupigia, Kuhesabia na Kujumlishia Kura. 
Kwa Upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Huduma za Sheria wa NEC, Bw. Emmanuel Kawishe amewaaeleza waandishi wa Habari kuwa kwa mujibu wa sheria mwenye mamlaka ya kumtangaza Mshindi ngazi ya Ubunge ni Msimamizi wa Uchaguzi na kwa ngazi ya Udiwani mwenye mamlaka ya kufanya hivyo ni Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi. 
Amesema kuwa zoezi la Kupiga Kura, Kuhesabu kura ,Kujumlisha Matokeo na Kutangaza matokeo litafanywa kwa uwazi na kwa kuzingatia Sheria na kutoa wito kwa wananchi wajitokeze kwa wingi kuwachagua viongozi wao. 
Amesema kuwa wananchi watakaoruhusiwa kupiga kura ni wale wenye sifa ambao watakuwa na kadi za kupigia kura na ambao majina yao yameonekana kwenye Daftari la kudumu la kupigia Kura na kusisitiza kwamba mwananchi ambaye jina lake halitakuwa kwenye Daftari la Kudumu la kupigia kura hataruhusiwa kupiga kura.

“Utaratibu wa kupiga kura umeelezwa katika Sheria, Ukisoma kifungu cha 63 kifungu kidogo cha 3 cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi A, kinaeleza wazi mwananchi anapofika kituoni alipopangiwa na Tume anaonyesha kadi yake ya kupigia kura na kisha jina lake linaitwa kwa sauti na ikiwa amekidhi sifa anaruhusiwa kupiga kura asipokidhi sifa Msimamizi wa Uchaguzi anayo Mamlaka ya kumzuia asipige Kura” Amesema.

No comments: