Friday, December 2, 2016

MAKATIBU 32 SHIRIKISHO LA VYUO VYA ELIMU YA JUU-CCM, WAPIGWA SEMINA KUWAJENGEA UWEZO

Shirikisho la Shirikisho la Vyuo vya Elimu ya Juu-CCM, limefanya semina ya utendaji kwa makatibu wake wote wa matawi katika mkoa wa Dar es Salaam, kwa lengo la kuwajengea uwezo katika kazi zao ili kuliimarisha Shirikisho na Chama Cha Mapinduzi.

Katibu Msaidizi wa CCM, Daniel Zenda alisema, katika semina hiyo iliyofanyia Novemba 30, mwaka huu, jumla ya Makatibu 32 walihudhuria na kuondoka wakiwa wameongeza upeo wao katika kazi zao za chama.

Alisema, moja ya mambo ambayo walifundwa Makatibu hao ni namna nzuri ya kuwezesha Chama Cha Mapinduzi kupata wanachama wapya miongoni mwa wanafunzi wa mwaka wa kwanza katika vyuo vikuu, kwa kuwa tegemeo na uhai wa Shirikisho hilo ni wanafunzi wa aina hiyo.

"Unajua Shirikisho linatilia mkazo sana katika kuhakikisha Makatibu wa Matawi wanashughulika kwa juhudi kubwa kuhakikisha kila wakati tunapata wanachama wapya hasa hawa wanaokuwa wanajiunga katika vyuo katika mwaka wa kwanza kwa kuwa hawa wanakuwa bado wabichi na wenye nguvu kutumikia Shirikisho na Chama kwa jumla", alisema Zenda na kuongeza..

"Shirikisho linalipa kipaumbele suala la kuingiza wanachama kutoka wale wa mwaka wa kwanza kwa sababu kuingia kwa wanavyuo wapya vyuoni kuna kuwa na maana pia kuwa wapo wanaondoka kutokana na kuhitimu masomo yao, ambao baada ya kuhitimu wanaweze kushindwa kuendelea kuwa wanachama wazuri wa shirikisho kutokana na kubanwa na shughuli nyingine".

Alisema, katika semina hiyo iliyofanyika Ukumbi wa Sekretarieti, Makao Makuu ya Umoja wa Vijana wa CCM, jijini Dar es Salaam, Makatibu wa matawi walihimizwa juu ya Wajibu wao, Muundo na wajibu wa kazi zao, Umuhimu wa Vikao na kujua tathmini ya  Wanachama Wapya.

Zenda alisema pia katika semina hiyo, makatibu walielimishwa namna bora ya utunzaji wa kumbukumbu na Taarifa za Vikao, Ufanyikaji wa Madarasa ya itikadi, Uzalendo na Maadili katika  ngazi ya Matawi na namna ya kufuatilia na kuwa tayari kusimamia vema chaguzi ndogo za kuziba nafasi zilizo wazi ndani ya Shirikisho.

Alisema, waliwataka Makatibu kufuatilia na kujua kwa undani changamoto zilizopo miongoni wa wanafunzi kuhusu mikopo, pia amesema walitakiwa kuhakikisha kila tawi kuwa na vitabu vya Katiba na Ilani ya CCM, na Kanuni za Shirikisho la Elimu ya Vyuo vya Elimu ya Juu-CCM.

Zenda alisema, pia waliwaelekeza Makatibu kujenga utaratibu wa kupokea maoni, Ushauri na Changamoto wanazokabiliana nazo wanafunzi na wanachama waliopo vyuoni kulingana na mazingira yaliyopo.
 Katibu Msaidizi wa CCM, Daniel Zenda akiongoza semina hiyo
🔺Washiriki wakiwa kwenye semina hiyo katika Ukumbi wa Sekretarieti, Makao Makuu ya Umoja wa Vijana wa CCM, jijini Dar es Salaam.

No comments: