Thursday, November 24, 2016

MTWARA, LINDI WAHIMIZWA KUIBUA FURSA ZA KUINUA MAISHA YA WANANCHI

 Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Bi.Halima Dendegu akizungumza jambo wakati wa ufunguzi wa semina ya siku moja ya mafunzo kwa viongozi wa mikoa ya Mtwara na Lindi kuhusuUratibu,usimamizi na ufuatiliaji wa utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Uwezeshaji wananchi kiuchumi ya mwaka 2004.  Mafunzo hayo yamefanyika mkoani Mtwara na kuratibiwa na Baraza la Taifa la Uwezeshaji wananchi kiuchumi (NEEC).
 Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) Bi.Beng’i Issa akifafanua jambo kwenye semina elekezi kwa viongozi wa mikoa ya Mtwara na Lindi kuhusu uratibu, usimamizi na ufatiliaji wa utekelezaji wa sera ya Taifa ya Uwezeshaji wananchi kiuchumi ya mwaka 2004. Kushoto kwake ni Katibu Tawala wa Mkoa wa Lindi, Bw .Ramadhani Kaswa.  Mkutano huo umefanyika mkoani Mtwara jana na kuratibiwa na NEEC.
Viongozi wa mikoa ya Mtwara na Lindi wakifatilia mada katika semina ya mafunzo juu ya uratibu, usimamizi na ufatiliaji wa utekelezaji wa sera ya Taifa ya Uwezeshaji wananchi kiuchumi ya mwaka 2004.  Mkutano huo ulifanyika jana Mkoani Mtwara na kushirikia Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri wa mikoa hiyo na Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC)

Na mwandishi wetu, Mtwara
 Viongozi wa Mikoa ya Mtwara na Lindi wametakiwa kutafsiri katika vitendo mafunzo kuhusu uratibu, usimamizi na ufuatiliaji wa utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ya Mwaka 2004 kwa kuwajengea uwezo wananchi katika kuibua fursa zitakazowaletea  maendeleo.


 Akishiriki katika mafunzo ya siku moja mjini hapa jana  juu ya utekelezaji wa sera ya uwezeshaji  iliyoratibiwa na Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi(NEEC), Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Bi Halima Dendegu, aliwambia viongozi kwamba mkoa hiyo miwili imejaliwa mambo mengi na kwa hiyo wananchi wanayo fursa ya kushinda umaskini iwapo wataongozwa vizuri.


“Tukatekeleze kwa vitendo elimu tunayoipata kutoka kwa wezeshaji wetu na ikawe na tafsiri halisi kwa wananchi katika maendeleo,” alisema Bi.Dendegu aliyefungua mkutano huo.


Amesema wajibu wa viongozi hao  ni  kuwachachua  kifikra wananchi katika maeneo yao  ili wawe wabunifu katika kuibua fursa na kuzifanyia kazi na wajipatie  maendeleo.



“Mafunzo haya yatajenga uelewa wa pamoja kwa viongozi na utekelezaji uwe wa pamoja katika mikoa yetu,” alisema  na kuongezea kuwa  mafunzo haya hayatakuwa na maana kama tafsiri yake haitaonekana kwenye ngazi ya jamii.



Bi.Dendegu alizitaja fursa zilizopo Mkoani Mtwara ambazo wananchi waongozwe kuzifaidi kuwa ni zao la korosho, gesi asilia, ardhi kwa kilimo, fukwe za Bahari ya Hindi, bandari na kiwanda cha cement cha Dangote , na kusema haya  ni maeneo ambayo wananchi wanaweza kubuni miradi itakayoendana na fursa hizo.



Alisema serikali itahakikisha kuchagua masoko ya bidhaa zitakazozalishwa na wananchi zinauzika kwa bei nzuri kama ilivyo katika zao la korosho kwa mwaka msimu huu.



Alishukuru NEEC kwa mikoa ya Mtwara na Lindi  na kuahidi kutoa ushirikiano ili kutimiza azma ya serikali ya kufikia uchumi wa kati.



 Katibu Mtendfaji wa NEEC, Bi.Beng’i Issa,  amesema madhumuni ya mafunzo haya ni kuwajengea uwezo Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri za mikoa hiyo miwili   juu ya sera ya uwezeshaji wananchi kiuchumi.



”Viongozi wengi ni wageni katika nyadhifa zao; hivyo  imetulazimu kutoa mafunzo haya ili kuwe na ushirikiano na waratibu wa madawati ya uwezeshaji katika ngazi za halmashauri,” amesema Bi.Issa



Amesifia  mwitiko wa wajumbe katika mafunzo haya  kwa kuwa viongozi wote wamehudhuria.


Mawazo ya wajumbe katika kuchangia mada yameboresha mikakati ya kuwawezesha wananchi kiuchumi, amesema na kuongeza kuwa  ushirikiano wa viongozi na wananchi ndio njia pekee ya kufika malengo ya kumuinua mwananchi kutoka  kipato cha chini na kufikia kipato cha kati.

 Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea,  Bi.Rukia Muwango, amesema mafunzo yatawasaidia viongozi  kuwajengea uwezo wananchi  juu ya dhana ya uwezeshaji.

Ameonyesha  na kusisitiza  umuhimu wa wananchi  kutunza fedha na kujiwekea akiba na kuwekeza katika fursa mbalimbali ili kukuza vipato vyao.


NEEC itaendelea kufanya mafunzo haya kwa kanda tano nchini ili viongozi wote wawe  na fafsiri moja katika dhana ya uezeshaji wananchi kiuchumi.

No comments: