Monday, November 21, 2016

Mtandao unaotetea marekebisho ya sheria usalama barabarani wawakumbuka wahanga wa ajali

Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA), Bi. Eda Sanga na msomaji wa taarifa ya pamoja ya Mtandao wa wadau kutoka asasi za kiraia unaotetea marekebisho ya sheria na sera ihusuyo usalama barabarani Tanzania akizungumza katika Siku ya Kimataifa Kuwakumbuka Wahanga wa Ajali za Barabarani inayoadhimishwa kila Novemba 20, 2016 Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA), Bi. Eda Sanga (katikati) na msomaji wa taarifa ya pamoja ya Mtandao wa wadau kutoka asasi za kiraia unaotetea marekebisho ya sheria na sera ihusuyo usalama barabarani Tanzania akizungumza katika Siku ya Kimataifa Kuwakumbuka Wahanga wa Ajali za Barabarani inayoadhimishwa kila Novemba 20, 2016. Kulia ni Jones John kutoka Taasisi ya Jukwaa la Haki za Watoto Tanzania na Mwakilishi kutoka TAWLA, Nasieku Kisamby (kushoto). Taasisi ya Jukwaa la Haki za Watoto Tanzania, Jones John (katikati) akizungumza katika Siku ya Kimataifa Kuwakumbuka Wahanga wa Ajali za Barabarani inayoadhimishwa kila Novemba 20, 2016 iliyofanyika Ofisi za TAMWA jijini Dar es Salaam. Kulia ni Bi. Gladness Munuo kutoka TAMWA


MTANDAO WA WADAU KUTOKA ASASI ZA KIRAIA UNAOTETEA MAREKEBISHO YA SHERIA NA SERA IHUSUYO USALAMA BARABARANI TANZANIA. SIKU YA KIMATAIFA KUWAKUMBUKA WAHANGA WA AJALI ZA BARABARANI 20 NOVEMBA, 2016.

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI Matukio ya ajali za barabarani yamekuwa na athari nyingi hapa nchini kiuchumi na kijamii. Vilevile matukio haya ya ajali za barabarani yamekuwa yakiwasababishia wananchi madhara makubwa yakiwemo kupoteza maisha, majeraha makubwa, ulemavu wa kudumu, mali kuharibika ikiwa ni pamoja na kuacha familia nyingi zikiwa tegemezi baada ya kuondokewa na watu wanaowategemea. 
 
Takwimu zinaonyesha kuwa takribani watu milioni 1.24 duniani hufariki kila mwaka kutokana na ajali za barabarani, aidha, watu milioni 20 mpaka 50 hupata ulemavu. (Hii ni kutokana na takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO). Kadhalika sehemu kubwa ya vifo na madhara ya ajali hizi zimetokea Kusini mwa Jangwa la Sahara , Tanzania ikiwa moja ya nchi hizo. 
 
Takwimu pia zinaonyesha kuwa ajali nyingi zinatokea kwa sababu ya makosa ya kibinadamu hasa uzembe wa madereva kutokutii sheria na kanuni za barabarani, ambapo kwa mujibu wa taarifa za jeshi la polisi nchini Tanzania, asilimia 76% ya ajali barabarani husababishwa na uzembe wa madereva, asilimia 8% husababishwa na ubovu wa barabara. Aidha ubovu wa vyombo vya moto husababisha ajali kwa asilimia 16%. 
 
Hata hivyo ajali nyingi zinaepukika kama madereva na watumiaji wengine wa barabara watazitii sheria na kanuni za Usalama barabarani. Kutokana na ajali hizo kuongezeka ndio maana ikatengwa siku maalum ya kimataifa ya kuwakumbuka waathirika wa ajali za barabarani kila mwaka ambayo huadhimishwa kila ifikapo tarehe 20 Novemba ya kila mwaka. Siku hii inatambulika kama siku rasmi ya kimataifa ya kuwakumbuka waathrika wa ajali hizo na familia zao na kuzitaka nchi wanachama pamoja na jumuiya za kimataifa kuitambua siku hiyo. 
 
Pia siku hiyo hutoa fursa kwa jamii nzima kukutana na kuwakumbuka wahanga wa ajali za barabarani ,kutafakari madhara, gharama, na hatua zinazoweza kuchukuliwa katika kuzuia ajali zisitokee. Vilevile siku ya kuwakumbuka wahanga wa ajali za barabarani inatoa nafasi kwa wadau kuikumbusha serikali wajibu wake na jamii nzima katika suala la kuzifanya barabara kuwa sehemu salama kwa kila mmoja. 
 
Hivyo basi mtandao wa wadau kutoka asasi za kiraia unaotetea marekebisho ya sheria na sera ihusuyo usalama barabarani Tanzania kama ambavyo unaratibiwa na Chama cha Wanawake Wanasheria (TAWLA) pamoja na mambo mengine katika kuadhimisha siku hii tunaisihi serikali na watunga sheria kuifanyia maboresho sheria ya Usalama barabarabi ya mwaka 1973 ili iweze kukabiliana ipasavyo na suala la ajali za barabarani pamoja na athari zinazotokana na ajali hizo Maeneo ndani ya sheria ambayo mtandao huu utajielekeza kuona sheria inafanyiwa mabadiliko/maboresho ni pamoja na;
 
Matumizi ya mikanda; Sheria ya sasa ya Usalama barabarani inasema ni kosa kisheria kwa dereva na abiria anayekaa kiti cha mbele kutokufunga mkanda wakati wa safari lakini sheria hiyo hiyo haisemi chochote kwa abiria wanaokaa kiti cha nyuma.

Utafiti uliofanywa na Shirika la Afya Duniani (WHO) unasema kuwa iwapo ajali ikitokea madhara/athari kwa abiria wa kiti cha mbele itapungua kwa 50% na kwa abiria wa nyuma madhara yatapungua kwa 70%. Kanuni zilizotungwa na SUMATRA zinataka abiria wote wafunge mkanda ila kwa vile sheria mama (Road Traffic Act of 1973) ipo kimya katika eneo hili utekelezaji wa kanuni unakuwa mgumu. Hivyo basi ni rai yetu sheria hiyo ibadilishwe na kuwataka abiria wote wanaokuwa katika chombo cha usafiri wa kibiashara au binafsi kufunga mkanda wakati wote wa safari. 

Matumizi sahihi ya kofia ngumu; Sheria ya sasa ya usalama barabarani inasema kuwa ni kosa kwa muendesha pikipiki kutokuvaa kofia ngumu wakati wa kuendesha chombo hicho. Lakini sheria hiyohiyo haisemii chochote kwa abiria anayepanda katika chombo hicho.

Vilevile pamoja na kuanishisha kosa kwa dereva wa pikipiki kutovaa kofia ngumu lakini pia sheria haielezi ni jinsi gani kofia inatakiwa kuvaliwa na aina maalum ya kofia inayotakiwa kuvaliwa. Kwa mujibu wa Utafiti wa Shirika la Afya Duniani (WHO) unaonyesha kuwa iwapo ajali itatokea madhara yanayotokea kwa kutovaa kofia maalum na kwa usahihi ni makubwa sana ukilinganisha na kofia hiyo ikivaliwa na kwa usahihi.
 
 Hivyo basi ukizingatia kuwa sasa hivi usafiri wa pikipiki umekuwa unatumika kwa kiasi kikubwa (public transport) hivyo ni rai yetu sheria hiyo ifanyiwe maboresho na kuweka kuwa ni sheria kwa mtu yoyote anayepanda pikipiki kuvaa kofia ngumu na kwa usahihi. 

Matumizi ya vilevi na uendeshaji vyombo vya usafiri: Sheria ya sasa ya usalama barabarani inasema kuwa itakuwa kosa kwa mtu yoyote kuendesha chombo cha moto akiwa na kiwango cha kilevi katika damu yake kinachozidi asilimia 0.08% katika mfumo wa mwili. 
 
Kiwango hiki ni kikubwa sana kikilinganishwa na tafiti zilizofanywa na Shirika la afya duniani na kupendekeza kiwango asilimia 0.05% kwa dereva aliyebobea (experienced driver) na asilimia 0.02% kwa dereva mchanga (young driver). Hivyo basi ni rai yetu kuwa sheria ifanyiwe marekebisho ili iendane na kiwango cha sasa cha kimataifa kilichofanyiwa utafiti. 

Mwendo kasi (Speeding): Mwendokasi umeendelea kuwa sababu kubwa ya ajali zinazogharimu uhai wa watu wengi. Sheria yetu inayo mapungufu kadhaa pamoja na juhudi nyingi za Jeshi la Polisi na wadau wengine kutaka kudhibiti jambo hili lemeendelea kuwa tatizo. Adhabu zisiszokidhi wala kuleta hofu kwa maderava wasiotaka kutii zimeendelea kufifisha juhudi za kudhibiti tatizo hili.

Tunatoa wito kwa watunga sera kutaka kujihulisha zaidi na wadu kuuelimisha umma zaidi katika eneo la uhusiano wa adhabu zitokanazo na makosa ya usalama barabarani na ongezeko la ajali. Pia sheria kufanyiwa maboresho na kuangalia kwa upya mianya iliyopo. Mwakilishi kutoka Chama cha wake Wanasheria Tanzania (TAWLA), Nasieku Kisamby (wa kwanza kushoto) akizungumza katika Siku ya Kimataifa Kuwakumbuka Wahanga wa Ajali za Barabarani inayoadhimishwa kila Novemba 20, 2016. Kutoka kulia ni Gladness Munuo, Jones John na Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA), Bi. Eda Sanga. Ofisa Mradi Msaidizi kutoka Tanganyika Law Society (TLS), Mabhezya Rehani akizungumza katika Siku ya Kimataifa Kuwakumbuka Wahanga wa Ajali za Barabarani inayoadhimishwa kila Novemba 20, 2016. Meza kuu ikiwa imesimama kwa dakika mbili kuwakumbuka watu waliopoteza maisha kutokana na ajali katika Siku ya Kimataifa Kuwakumbuka Wahanga wa Ajali za Barabarani inayoadhimishwa kila Novemba 20, 2016. Christina Thomas mkazi wa Kibaha na mmoja wa waathiriwa wa ajali za barabarani akizungumza katika Siku ya Kimataifa Kuwakumbuka Wahanga wa Ajali za Barabarani inayoadhimishwa kila Novemba 20, 2016 iliyofanyika Ofisi za TAMWA jijini Dar es Salaam. Salum Juma Haji (kulia) makazi wa Buguruni jijini Dar es Salaam akizungumza jambo katika Siku ya Kimataifa Kuwakumbuka Wahanga wa Ajali za Barabarani inayoadhimishwa kila Novemba 20, 2016. Mkutano kati ya wanahabari kutoka vyombo mbalimbali vya habari pamoja ya Mtandao wa wadau kutoka asasi za kiraia unaotetea marekebisho ya sheria na sera ihusuyo ukiendelea.

No comments: