Friday, November 25, 2016

ENG. NGONYANI AZINDUA SAFARI ZA NDEGE YA ATCL KIGOMA

 Mkuu wa Bandari ya Kigoma Bw. Athuman Mwaibamba akijadiliana jambo na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani alipoitembelea bandari ya Kigoma kukagua utendaji kazi wa bandari hiyo.
 Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani akifafanua jambo kwa wafanyakazi wanaopakia na kushusha mizigo katika bandari ya Kigoma.
 Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani akisikiliza changamoto zinazowakabili abiria wanaotumia treni ya reli ya kati katika stesheni ya Kigoma.
 Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani akipata ufafanuzi kutoka kwa Kaimu mkuu wa Shirika la Posta Mkoa wa Kigoma Bw.Juma Kaungenge wakati alipokagua huduma za posta katika mkoa huo.
 Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani akitoa maelekezo kwa viongozi wa uwanja wa ndege na Mamlaka ya anga Mkoani Kigoma namna ya kuhudumia ndege ili kuvutia idadi ya abiria.
Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani akiwaaga viongozi na watendaji wa taasisi zilizo chini ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano  Mkoani Kigoma mara baada ya kuzindua safari za ndege Bombadier Q400 toka Kigoma kwenda Dar es salaam. Picha na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano -WUUM


Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani amewataka wakazi wa mikoa ya Kigoma, Katavi na Rukwa kuwekeza katika biashara na vivutio vya utalii ili kunufaika na fursa ya ujio wa Ndege mpya za Shirika la ndege Tanzania (ATCL) katika kanda hiyo.

Akizungumza wakati wa kuzindua usafiri wa ndege ya ATCL kutoka Kigoma kwenda Dar es salaam Eng.Ngonyani amesema Serikali itahakikisha inaufufua ukanda wa magharibi mwa Tanzania kwa kuimarisha barabara za lami na kuwa na safari za ndege za uhakika ili kuvutia watalii kutembelea vivutio hivyo na hivyo kukuza uchumi wa mikoa hiyo.

“Kwa kuanza ATCL itakuwa na safari nne kwa wiki kuja Kigoma na idadi ya abiria ikiwa ya kutosha tutaziongeza ili kuwawezesha wasafiri na wadau wengine wa utalii kufika Kigoma kwa urahisi”, Amesema Eng. Ngonyani.
Amewataka wafanyakazi wa ATCL na viwanja vya ndege nchini (TAA), kuwa wabunifu ili kuvutia abiria wengi na hivyo juhudi za Serikali za kuiunganisha nchi kwa usafiri wa  anga zifanikiwe katika muda mfupi.

“Serikali tutaendelea kuongeza ukubwa wa uwanja wa ndege wa Kigoma na Mpanda na kutoza gharama nafuu ili kuwezesha ndege nyingi kutua katika ukanda wa Ziwa Tanganyika na kuwezesha abiria na watalii wengi kunufaika na usafiri wa anga,”. Amesisitiza  Eng. Ngonyani.

Katika hatua nyingine Naibu Waziri Ngonyani amemuagiza Mkuu wa Stesheni ya reli Kigoma Bw. Ally Shamte na Mkuu wa Bandari ya Kigoma Bw. Athumani Mwaibamba kutengeneza mkakati wa pamoja utakaowezesha bandari ya Kigoma kupata mizigo mingi kutoka katika nchi za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Burundi na hivyo kuwezesha biashara ya uhakika kufanyika katika bandari hiyo.“Angalieni soko lilivyo na jinsi  soko linavyobadilika, hakikisheni mnaongeza wateja na kuongeza ubunifu ili watu wavutike kutumia bandari yetu”. Amesisitiza Eng. Ngonyani.

Naibu Waziri huyo amesema Serikali itaendelea na jitihada za kuboresha miundombinu ya reli na bandari hivyo kazi ya watendaji iwe ubunifu wa kibiashara ili kuiwezesha Serikali kupata faida.

Mwenyekiti wa taasisi zilizo chini ya wizara ya ujenzi,uchukuzi na mawasiliano ambae pia ni Meneja wa Wakala wa Barabara mkoa wa Kigoma (TANROADS) eng. Narcis Choma amemhakikishi Naibu Waziri Ngonyani kuwa wamejipanga kuhakikisha wanaboresha miundombinu ya mkoa wa Kigoma ili kukuza uchumi wa watu wa  kanda ya magharibi.

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.



No comments: