Thursday, October 13, 2016

Waziri Muhongo akutana na Balozi Mpya wa Canada nchini



Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (katikati) akiwa na Balozi Mpya wa Canada nchini, Ian Myles (kushoto) na Kamishna wa Biashara katika Ubalozi huo, Anita Kundy mara baada ya kumaliza kikao kilichofanyika katika Ofisi za Wizara ya Nishati na Madini jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (kulia) akiwa na Balozi Mpya wa Canada nchini, Ian Myles mara baada ya kumaliza kikao kilichofanyika katika Ofisi za Wizara ya Nishati na Madini jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (kulia) akijadiliana jambo na Balozi Mpya wa Canada nchini, Ian Myles wakati wa kikao kilichofanyika katika Ofisi za Wizara ya Nishati na Madini jijini Dar es Salaam.
Balozi Mpya wa Canada nchini, Ian Myles akitia saini katika kitabu cha Wageni mara baada ya kumaliza mazungumzo na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (kulia) jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Kamishna wa Biashara katika Ubalozi huo, Anita Kundy .
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (katikati) akiwa katika kikao na Balozi Mpya wa Canada nchini, Ian Myles (kulia kwa Waziri ) na Kamishna wa Biashara katika Ubalozi huo, Anita Kundy (kulia kwa Balozi). Kikao hicho kilifanyika katika Ofisi za Wizara ya Nishati na Madini jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na watendaji wa Wizara na Taasisi zake. Kushoto kwa Waziri ni Kaimu Kamishna wa Nishati, Mhandisi Innocent Luoga na wa kwanza kushoto ni Kaimu Kamishna wa Madini, Julius Sarota.












Waziri Muhongo akutana na Balozi Mpya wa Canada nchini
ΓΌ Wazungumzia uendelezaji Chuo cha Madini, Miradi ya Nishati na Madini



Na Teresia Mhagama

Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amekutana na Balozi Mpya wa Canada nchini, Ian Myles kuzungumzia masuala mbalimbali ya uendelezaji wa Sekta za Nishati na Madini nchini.

Kikao hicho kilifanyika katika Ofisi za Wizara ya Nishati na Madini jijini Dar es Salaam ikiwa ni mara ya kwanza kwa Balozi huyo kufika wizarani tangu alipowasili nchini mwezi Agosti mwaka huu ili kuiwakilisha nchi ya Canada.

Awali Balozi Myles alimweleza Profesa Muhongo kuwa nchi hiyo imeshiriki katika shughuli mbalimbali za uendelezaji wa sekta za Nishati na Madini nchini.

Mathalani, kupitia Shirika la Maendeleo la Canada (CIDA) nchi hiyo ilikuwa ikitoa fedha kwa Wakala wa Ukaguzi wa Madini nchini (TMAA) katika mwaka wa Fedha wa 2012/2013 hadi 2015/2016 ili kuuwezesha Wakala huo kufanya shughuli zake za ukaguzi kwa ufanisi pamoja na kujengewa uwezo kupitia mafunzo ambapo jumla ya fedha zilizotolewa ni Dola za Canada 2500.

"Katika Mpango wa Uhamasishaji Uwazi katika Mapato ya Madini, Gesi Asilia na Mafuta (TEITI), Canada ilishiriki katika kusaidia mchakato wa maandalizi ya kupata Sheria ya kuongoza Tasnia ambayo ilipitishwa na Bunge mwaka 2015. Pia tunawajengea uwezo wataalam ili waweze kufanya kazi zao kwa ufanisi," alisema Balozi Myles

Aidha, alisema kuwa Tanzania ni moja ya nchi zinazopewa kipaumbele na Serikali ya Canada katika masuala mbalimbali ikiwemo utoaji wa misaada ya kifedha.

kwa upande wake Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, alisema kuwa uhusiano kati ya nchi hizo mbili ulianza tangu miaka ya 1960 na kwamba nchi hizo zimekuwa zikishirikiana katika masuala mbalimbali ikiwemo Kilimo na Elimu.

Alisema kuwa katika Sekta ya Madini, kampuni kubwa zinazofanya shughuli za uchimbaji wa madini nchini, nyingi zinatoka nchini Canada na kutoa mfano wa kampuni ya uchimbaji madini ya Acacia na kwamba kodi zinazolipwa na kampuni hizo kwa Serikali, zinasaidia kuendeleza miradi mingine ya maendeleo.

Kuhusu uendelezaji wa Chuo cha Madini Dodoma (MRI), Profesa Muhongo alimweza Balozi Myles kuwa mazungumzo kati ya Wizara na Ubalozi huo kuhusu kukiendeleza Chuo hicho kuwa katika ngazi ya Polytechnic yalikwishaanza hivyo alimweleza Balozi huyo kuwa ni vyema utekelezaji wa suala hilo ukaanza.

" Tunataka Chuo hiki kiwe cha kimataifa, kisiwe kinatambulika hapa nchini tu na pia kiwe kinabadilishana wataalam na Vyuo vingine vya nje ili kuboresha elimu inayotolewa katika Taasisi hiyo na pia kijitegemee, badala ya kuwa chini ya mwavuli wa Wizara ya Nishati na Madini,” alisema Profesa Muhongo.

Aidha alitumia fursa hiyo kuwaalika Wawekezaji kutoka Canada kuja kuwekeza katika utafiti na uchimbaji wa madini ya metali aina graphite na lithium kutokana na umuhimu wake duniani na kutoa mfano kuwa madini ya graphite yanatumika kutengeneza vitu mbalimbali ikiwemo betri.

"Madini haya ya metali yana umuhimu sana kwa sasa mfano ifikapo mwaka 1920-40 asilimia 40 ya magari duniani yatakuwa yakitumia umeme hivyo ili kuwezesha hilo wanahitaji madini haya," alisema Profesa Muhongo

Pia alizialika kampuni za Canada kuja kuwekeza katika uchimbaji wa madini adimu (rare metals) ambayo yanahitajika katika teknolojia ya kisasa kama vile madini ya titanium ambayo yanatumika katika kutengeneza mitambo mbalimbali ikiwemo inayotumika kuzalishia umeme.

Pamoja na kualika makampuni ya Canada kuja kuzalisha umeme nchini, Profesa Muhongo alitumia fursa hiyo kumueleza Balozi Myles ombi la Tanzania la kupeleka wataalam wake nchini Canada kusomea masuala ya mafuta na gesi.

No comments: