Thursday, October 6, 2016

WANANCHI WAHAMASISHWA KUSHIRIKI KILELE CHA MBIO ZA MWENGE WA UHURU MKOANI SIMIYU

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony J. Mtaka akizungumza na waandishi wa habari juu ya Kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru, Kumbukumbu ya kifo cha Baba wa Taifa na Maadhimisho ya Wiki ya Vijana Oktoba 14 mwaka 2016,  yatakayofanyika mkoani humo.
 Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony J. Mtaka akizungumza na waandishi wa habari juu ya Kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru, Kumbukumbu ya kifo cha Baba wa Taifa na Maadhimisho ya Wiki ya Vijana Oktoba 14 mwaka 2016,  yatakayofanyika mkoani humo.  
Baadhi ya vijana wa Wilaya ya Maswa wakiwa katika zoezi la uzalishaji chaki katika kiwanda cha kutengeneza chaki kilichopo wilayani humo ambacho kinazalisha chaki zinazotambulika sokoni kama Mzinazotumika mkoani Simiyu.
Baadhi ya vijana wa Wilaya ya Meatu wakielekezwa namna ya kupima maziwa na kutambua maziwa bora yasiyo na maji, katika kiwanda chao cha uzalishaji wa maziwa yanayotambulika sokoni kama ‘MEATU MILK’
Sehemu ya Jengo la Ofisi ya Vijana wa Wilaya ya Meatu wanaojishughulisha na usindikaji wa maziwa (MEATU MILK).


Na Stella Kalinga, Simiyu

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka ametoa wito kwa wananchi wa Mkoa wa Simiyu na Taifa kwa ujumla kushiriki katika Kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru, Kumbukumbu ya kifo cha Baba wa Taifa na Maadhimisho ya Wiki ya Vijana mwaka 2016,  yatakayofanyika mkoani humo.


Akizungumza na waandishi wa Habari Ofisini kwake Mtaka amesema Mkoa wa Simiyu umepewa heshima ya kuwa mwenyeji wa Kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru, Kumbukumbu ya kifo cha Baba wa Taifa na Maadhimisho ya Wiki ya Vijana yatakayofanyika Oktoba 14, 2016 katika Uwanja wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi.


Mtaka ameeleza kuwa Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli ambaye  pia atashiriki Ibada ya Kumbukumbu ya Kifo cha Baba wa Taifa, Mwl. Julius Kambarage Nyerere, itakayofanyika siku hiyo ya tarehe 14 Oktoba, 2016 katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Yohana, Mjini Bariadi kuanzia saa 1:00 kamili asubuhi.


Wakati huo huo Mtaka amesema maadhimisho ya wiki ya vijana yatafunguliwa rasmi tarehe 08 Oktoba, 2016 na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye ulemavu, Mhe. Jenista Mhagama (Mb) katika Uwanja wa SABASABA Mjini Bariadi; ambapo shughuli mbalimbali za vikundi vya maendeleo ya vijana kutoka Halmashauri zote nchini zikiwemo za ujasiriamali pamoja na ugunduzi wa kisayansi ambao umethibitishwa na Tume ya Taifa ya Sayansi zitaoneshwa katika mabanda maalum yaliyojengwa katika uwanja huo.


 “Kwa upande mkoa wa Simiyu vikundi vyetu vya vijana vimejiandaa kuonesha shughuli mbalimbali za kiuchumi zinazofanywa katika Halmashauri husika;ambapo kimkoa tunatekeleza mkakati wa kila wilaya kuzalisha bidhaa/huduma moja yaani (one district one product).  

Kulingana na mkakati huo Vijana wa Wilaya ya Meatu wameanzisha kiwanda cha kusindika maziwa ya ng’ombe, Maswa kiwanda cha kuzalisha chaki na wilaya nyingine tunaendelea kujipanga kuzalisha bidhaa nyingine” alisema Mtaka.


Aidha, Mtaka amewakumbusha wananchi wa Mkoa wa Simiyu kuwa Maadhimisho haya ni fursa kwao kiuchumi na kijamii kwa kuwa watapokea wageni wengi kutoka maeneo mbalimbali nchini ambao watahitaji malazi, chakula na huduma nyingine muhimu, hivyo waoneshe ukarimu na ushirikiano wa hali ya juu ili kuupa heshima mkoa huo.


Naye Pendo Benjamin Mkazi wa Mtaa wa Sima mjini Bariadi amesema amepokea kwa furaha suala la kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru kufanyika mkoani Simiyu kwa kuwa ni la kihistoria, pia ni fursa kwa wafanyabiashara wa vyakula, nyumba za kulala wageni na mahitaji mengine.


Sanjali na hilo Mkuu wa Mkoa wa Simiyu ametoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi kuchangia damu kwa hiari katika uwanja wa SABASABA kuanzia tarehe 08/10/2016 hadi 13/10/2016, zoezi ambalo litafanywa na Hospitali Teule ya Rufaa ya Mkoa kwa kushirikiana na Shirika la Msalaba Mwekundu na Shirika la AGPAHI  kwa ajili ya kuwasaidia watu wenye uhitaji wa damu hususani mama wajawazito, majeruhi wa ajali na watoto wenye umri chini ya miaka mitano.


Kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru, Kumbukumbu ya kifo cha Baba wa Taifa na Maadhimisho ya Wiki ya Vijana kwa mwaka 2016 ni tukio la kihistoria kwa Mkoa wa Simiyu na la kwanza kwa Mhe.Rais wa awamu ya tano tangu alipopata ridhaa ya wananchi kuliongoza Taifa letu.

No comments: