Wednesday, October 5, 2016

JAFO AWACHARUKIA MAAFISA ELIMU NCHINI WENYE TABIA YA KUSHINDA OFISINI BILA YA KWENDA VIJIJINI.

 Naibu waziri ofisi ya Rais Tamisemi kushoto Seleman Jafo akipena mikono na Mwenyekiti wa umoja wa wafanyabiashara wa mazao ya misitu Wilaya ya Kisarawe,(UWAMAMI) baada ya hafla fupi ya kukabidhiana madawati 150 yenye thamani ya kiasi cha shilingi milioni 15.
 Naibu waziri ofisi ya Rais Tamisemi akizungumza na watendaji wa halmashauri ya wilaya ya Kisarawe mara baada ya kupokea msaada wa madawati 150 kwa ajili ya kuwasaidia wanafunzi kuondokana na tatizo la kukaa chini (PICHA ZOTE NA VICTOR MASANGU)

NA VICTOR MASANGU, KISARAWE.
NAIBU waziri ofisi ya rais  Tamisemi Selaman Jafo amewaagiza maafisa elimu wa shule za sekondari na msingi hapa nchini  kuachana na tabia ya kufanya kazi kwa mazoea ya kushinda wakiwa wamekaa ofisini tu bila ya kujishughulisha na badala yake wanapaswa kuhakikisha wanakwenda katika maeneo ya kazi hususan ya vijijini kwa ajili ya kuweza kubaini changamoto mbali mbali  zinazoikabili sekta ya elimu ikiwemo upungufu wa madawati, vyoo pamoja na madarasa.

Jafo ametoa agizo hilo wakati wa hafla fupi ya kukabidhiwa madawati 150 kwa niaba ya serikali  katika halmashauri ya Wilaya ya Kisarawe Mkoa wa Pwani yaliyotolewa na umoja wa wafanyabiashara wa mazao ya misitu (UWAMAMI) iliyofanyika wilayani humo.

Alisema kwamba kuna baadhi ya maafisa elimu hawatambua majukumu yao ipasavyo hivyo  kutokana na agizo lililotolewa na  Rais Dr. John Magufuli la wanafunzi wote kusoma wakiwa wamekaa chini ya madawati atahahakikisha anawavalia njunga watendaji wote  watakaobainika wanakwamisha kwa makusudi  juhudi za serikali katika kuwaletea wananchi maendeleo.

“Kwa kweli kuna baadhi ya maafisa elimu wengine wana tabia ya kukaa tu mezani hawaendi kujishughulisha na kuangalia changamoto za vijijini, ili kuweza kuzitafutia ufumbuzi na kuweka mikakati ya kuboresha sekta ya elimu hapa nchini kwa hiyo ninawaomba sana tucahpe kazi kwa bidii, ili tuweze kuleta maendeleo ya elimu,”alisema Jafo.

Aidha Jafo baada ya kukabidhiwa msaada huo wa madawati  amebainisha kuwa licha ya utekelezaji wa agizo la rais la utengenezaji wa madawati  kwa halmashauri zote nchini kufikia kiwango cha asilimia 98 hadi sasa, lakini bado kuna  changamoto nyingine ya uhaba ma madarasa,matundu ya vyoo pamoja na nyumba za kuishi walimu.

Kwa upande wake Katibu mkuu  wa umoja wa wafanyabiashara wa mazao ya misitu Wilaya ya Kisarawe (UWAMAMI) Ally Kombe alisema wameamua kutoa  madawati hayo yaliyotokana na miti waliyoipanda na kuivuna   kwa lengo la kuweza kuunga juhudi za serikali katika kuhakikisha wanafunzi wote wa shule za msingi na sekondari wanasoma wakiwa kwenye madawati ili kuongeza kiwango cha ufaulu.

Katibu huyo alifafanua kwamba msaada huo utaweza kuwa mmkombozi mkubwa wa wanafunzi wanaosoma katika wilaya ya kisarawe na kuwaomba wayatunze  kwa hali na mali madawati hayo ii yaweze kutumika katika vizazi vijavyo.
Naye Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Wilaya ya Kisarawe  Musa Gama amebainisha kuwa licha ya kupatiwa madawati hayo lakini bado wanakabiliwa na upungufu wa madawati mengine   404 hivyo kunahitajika juhudi za makusudi ili kuweza kuondoka na changamoto ya wanafunzi kusoma wakiwa katika mlundikano na baadhi yao kukaa chini ya sakafu.

CHANGAMOTO ya kuwepo kwa  upungufu wa madawat katika shule za msingi na sekondari katika baadhi ya maeneo bado inaonekana kuwa ni tatizo licha ya agizo lililotolewa na Rais wa awamu ya tano Dr.John Magufuli ya kuziagiza halmashauri zote nchini kuhakikisha inataengeneza madawati ili wanafunzi waondokana na kero ya kusoma wakiwa wamekaa chini ya sakafu.

No comments: