Sunday, October 30, 2016

CODERT yajipanga kuinua maisha ya wananchi 7000 Geita

Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO, Geita

Shirika la Misaada na Maendeleo ya Jamii (CODERT) limejipanga kuwasaidia jumla ya wananchi 7000 wanaoishi katika mazingira magumu Mkoani Geita ili waweze kujikwamua kutoka katika lindi la umasikini linalowakabili.

Shirika hilo ni moja ya mashirika yanayoshirikiana na Shirika la Plan International katika kutekeleza Mradi wa Uondoaji Ajira Hatarishi na Vitendo vya Ukatili kwa Watoto unaofadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Ufaransa (AFD) na kuratibiwa na shirika la plan International kwa kuwapatia wananchi hao vifaa pamoja na elimu ya ujasiriamali.


Hayo yamesemwa leo Mkoani Geita na Msimamizi wa Miradi wa shirika hilo,  Edward Saramba alipokuwa akiongea na waandishi wa habari kuhusu njia wanazozitumia kuwainua wazazi na vijana wa mkoa huo ili waache kuwapeleka watoto walio na umri chini ya miaka 18 kufanya kazi katika maeneo ya migodi.

Saramba amesema kuwa mradi huo unaoratibiwa na shirika la Plan International umewasaidia wananchi wa mkoani Geita kuinua maisha yao kwa kuwasaidia kuunda vikundi vya kuweka na kukopa pamoja na kuwapatia vifaa mbalimbali vinavyowawezesha kujipatia vipato ambavyo vinawasaidia kuendesha maisha yao ya kila siku.

“Awamu ya kwanza ya mradi huu iliisha Novemba 2015 na tulifanikiwa kuwafikia wananchi wenye mazingira magumu zaidi ya 4000 waishio katika Wilaya za Nyan’ghwale na Geita, kwa awamu hii tumeongeza wilaya ya Chato hivyo tumejipanga kuwafikia wananchi 7000 tukiamini kuwa kuwasaidia wananchi hao kutapunguza ajira hatarishi kwa watoto”, alisema Saramba.

Amevitaja baadhi ya vifaa walivyovitoa kwa wananchi wanaoishi kwenye mazingira magumu kuwa ni mashine za kujazia upepo magari na pikipiki (compressor), vyerehani, mabomba ya maji, mizinga ya nyuki, viti na meza kwa mama lishe, kuwapatia wafugaji kuku pamoja na mbegu za mahindi na mpunga kwa wakulima, zaidi ya hayo waliweza kufadhili mafunzo ya kutengeneza baiskeli, pikipiki na cherehani.

Kwa upande wake mmoja wa wananchi waliosaidiwa kupitia Mradi huo, Shabani Masanja ameyashukuru mashirika hayo kwa sababu kabla ya mradi huo kumfikia alikua na maisha magumu lakini baada ya kuanza ufugaji wa kuku aliopewa kutoka katika shirika hilo ameona tofauti kubwa ya maisha.

“Nashukuru sana mashirika yaliyoniwezesha kwa sababu yameninufaisha, kwa sasa ninaweza nikauza kuku na mayai vinavyoniwezesha kusomesha watoto wangu, kununua chakula, nimeweka umeme kwenye nyumba yangu ambao unanisaidia kufanya ufugaji wa kisasa kwa sababu mwanzoni nilikua nikikuza vifaranga kwa kuwawekea moto lakini sasa hivi natumia umeme kuwakuza”, alisema Masanja.

Mmoja wa wananchi waliosaidiwa kupata mradi wa kuku kupitia Mradi wa Uondoaji wa Ajira Hatarishi na Vitendo vya Ukatili kwa Watoto unaofadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Ufaransa (AFD), unaratibiwa na Shirika la Plan International na kutekelezwa katika Wilaya 3 za Mkoa wa Geita, Shabani Masanja akiongea na waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu mradi huo ulivyomsaidia. 

Msimamizi wa Miradi wa Shirika la Misaada na Maendeleo ya Jamii (CODERT), Edward Saramba alipokuwa akiongea na waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu njia wanazozitumia kuwainua wazazi na vijana wa Mkoa wa Geita ili waache kuwapeleka watoto walio na umri chini ya miaka 18 kufanya kazi katika maeneo ya migodi.

No comments: