Saturday, October 22, 2016

BAADA YA TAMKO LA SERIKALI WATUMISHI WAFURIKA VITUO VYA USAJILI


Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Meja Jenerali Projest Rwegasira akipokea ripoti ya utekelezaji wa zoezi la Usajili watumishi wa Umma toka kwa Afisa Usajili mkoa wa Dodoma Bwana Khalid Mrisho.

Afisa Utawala Bi. Salma Mohamed toka ofisi ya Wakala wa Geolojia (GST) akihakiki orodha ya watumishi wake ambao hawajasajiliwa Vitambulisho vya Taifa, kufuatia agizo la Serikali la kila mtumishi wa Umma kuwa amesajiliwa kufikia Oktoba 31, 2016. Pembeni ni Bi.Rehema Kionaumela Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Uratibu Wilaya NIDA

Afisa Usajili NIDA Bw. Devis Lubago, akimsajili na kuchukua alama za kibaiolojia mtumishi wa Umma aliyefika ofisi za NIDA Dodoma kukamilisha usajili.

Mmoja wa Watumishi wa Umma akichukuliwa alama za vidole wakati wa zoezi la usajili Watumishi wa Umma linaloendelea mkoani Dodoma.


Baadhi ya watumishi wa Umma wakisubiri kupata huduma ya usajli kwenye ofisi ya NIDA, jengo la Hazina mkoani Dodoma

Afisa Usajili Bi. Lucina Ramadhani akikagua taarifa za mtumishi kabla ya kuanza kuingiza taarifa zake kwenye mfumo

Bi. Aziza Konyo mmoja wa watumishi wa Umma akichukuliwa alama za vidole alipofika kusajiliwa katika zoezi linaloendelea nchi nzima la kusajili Watumishi wa Umma.

Watumishi wa Umma mkoani Dodoma wamefurika katika vituo vya usajili kufuatia tamko la Serikali la kuongeza muda wa usajili Vitambulisho vya Taifa kufikia Oktoba 31, 2016 ambapo mfanyakazi au mwajiri ambaye atashindwa kutekeleza agizo hilo hatua stahiki zitachukuliwa dhidi yake; tamko lililotolewa na Waziri ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora alipokutana na vyombo vya habari hivi karibuni.

Watumishi waliojitokeza katika vituo wameonekana kuwa tayari wamejaza fomu za maombi ya Vitambulisho vya Taifa wakiwa wamejipanga kupigwa picha.

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi amekuwa miongoni mwa viongozi waliotembelea moja wapo ya vituo vya usajili mkoani Dodoma; kushuhudia namna shughuli za usajili zinavyofanyika na kupata taarifa ya mpango wa utekelezaji zoezi hilo ilivyopangwa na mkoa husika, katika kuhakikisha zoezi hilo linakamilika kwa wakati na kila mtumishi anasajiliwa na kuchukuliwa alama za Vidole, saini ya kielektroniki na picha.

Zoezi la Usajili Watumishi wa Umma linaenda sambamba na kuanza kwa uhakiki wa taarifa za uraia wa waombaji wote walioomba kupatiwa Vitambulisho vya Taifa.

Tayari mikoa ambayo usajili umekamilika, zoezi la uhakiki wa taarifa na mapingamizi linaanza mara moja ili vitambulisho kuanza kuzalishwa.

No comments: