Saturday, September 10, 2016

MKUU WA MKOA WA MWANZA AKABIDHI VYAKULA KWA NIABA YA RAIS MAGUFULI KWENYE KITUO CHA WAZEE BUKUMBI KWA AJILI YA IDD EL HAJJ.


Katika kusherehekea Sikukuu ya Idd El Hajj siku ya Jumatatu Septemba 12, 2016, Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt.John Pombe Magufuli, ametoa msaada wa vyakula wenye thamani ya shilingi laki saba na elfu themanini (780,000), kwa ajili ya Kituo cha kulelea Wazee na Walemavu wasiojiweza cha Bukumbi Wilaya ya Misungwi mkoani Mwanza.

Akikabidhi msaada huo jana, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella, aliuhimiza uongozi wa kituo hicho kusimamia vyema ugawaji wa vyakula hivyo li kuwafikia walengwa, ikizingatiwa kwamba kumekuwa kukiibuka malalamiko kutoka kwa wazee wanaoishi katika kituo hicho kwamba misaada ambayo imekuwa ikitolewa na serikali pamoja na wafadhili mbalimbali imekuwa haiwafikii yote.

Hata hivyo Kaimu Afisa Mfawidhi wa kituo hicho, Georgina Kwesigabo, alitanabaisha kwamba vyakula na misaana ambayo imekuwa ikitolewa na serikali pamoja na wafadhili mbalimbali kituoni hapo, yote imekuwa ikiwafikia walengwa wote isipokuwa kuna changamoto ya baadhi yao kuuza misaada wanayopatiwa ikiwemo vyakula, jambo ambalo linaulazimu uongozi wa kituo hicho kuandaa utaratibu wa kusimamia misaada hiyo hususani kuwapikia chakula wanaoishi kituoni hapo badala ya kuwagawia chakula ili wajipikie wenyewe.

Wazee wanaoishi kituoni hapo waliishukuru serikali kwa msaada huo ambapo walisema wanaendelea kumuombea Rais Magufuli na Serikali yake ili iendelee kuboresha kituo hicho ikiweo kuwekewa uzio ili kuondokana na hofu ya kiusalama waliyonayo kwani wakati mwingine wamekuwa wakiibiwa mali zao ikiwemo kuku ambazo wamekuwa wakizifuga.

Vyakula vilitolewa na Mhe.Rais Magufuli ni, mchele gunia sita (kila gunia kilo 50), mafuta ya kupikia madumu manne (kila dumu lita 20) pamoja na mbuzi wawili.
Baadhi ya wazee wanaoishi kwenye Kituo cha Bukumbi, wakifurahia mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza baada ya Rais Magufuli kuwapatia msaada wa vyakula kwa ajili ya kusherehekea Sikukuu ya Idd El Hajj, itakayofanyika kesho kutwa jumatatu.
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe.John Mongella (mwenye kofia), akimsikiliza mmoja wa wazee katika Kituo cha Wazee Bukumbi.
Mmoja wa akina mama kwenye Kituo cha Bukumbi akiishukuru Serikali kwa msaada wa chakula ilioutoa kituoni hapo
Mkuu wa Wilaya ya Misungwi, Mhe.Juma Sweda (kulia), akizungumza wakati wa kukabidhi msaada wa chakula uliotolewa na Mhe.Rais Magufuli katika Kituo cha Wazee Bukumbi wilayani humo. Alisema Serikali inawajali Wazee wanaoishi katika kituo hicho na kwamba ina upendo kwao ndiyo maana inaendelea kuwahudumia.
Kaimu Afisa Mfawidhi wa kituo hicho, Georgina Kwesigabo, alitanabaisha kwamba vyakula na misaana ambayo imekuwa ikitolewa na serikali pamoja na wafadhiri mbalimbali kituoni hapo, yote imekuwa ikiwafikia walengwa wote isipokuwa kuna changamoto ya baadhi yao kuuza misaada wanayopatiwa ikiwemo vyakula, jambo ambalo linaulazimu uongozi wa kituo hicho kuandaa utaratibu wa kusimamia misaada hiyo hususani kuwapikia chakula wanaoishi kituoni hapo badala ya kuwagawia chakula ili wajipikie wenyewe.
Vyakula vilivyotolewa na Mhe.Rais Magufuli kwa ajili ya Makao ya Wazee na walemavu wasiojiweza Bukumbi, Wilaya ya Misungwi mkoani Mwanza.
Huyu mbuzi, tehe tehe tehe!!
Makao ya Wazee na walemavu wasiojiweza Bukumbi, Wilaya ya Misungwi mkoani Mwanza.

Imeandaliwa na George Binagi-GB Pazzo wa BMG

No comments: