Saturday, July 30, 2016

Wafanyakazi Muhimbili Waongeza Mapato Hadi Kufikia Sh 4.8 Bilioni


Na John Stephen, MNH .

Dar es Salaam. Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) imefanikiwa kuongeza mapato kutoka Sh 2.3 bilioni yaliyokuwa yakikusanywa Desemba mwaka jana hadi kufikia Sh 4.8 bilioni Mei mwaka huu. 

Hayo yamesemwa LEO na Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali hiyo, Profesa Lawrence Museru wakati hafla ya kutunuku vyeti kwa wafanyakazi bora wa hospitali hiyo.
Hospitali hiyo imefanikiwa kuongeza mapato kutokana na juhudi za wafanyakazi ambao wanafanya kazi kwa ari kubwa ili kutoa huduma bora kwa wagonjwa. 
Pia, wafanyakazi wamehamasika kutokana na mkurugenzi huyo kuwajali wafanyakazi na kusikiliza kero na kuzitatua kwa wakati kwa mfano hivi karibuni alilipa malimbikizo ya wafanyakazi. Profesa Museru amesema mapato hayo yameongezeka kutokana na juhudi za wafanyakazi ambao wamekuwa wakifanya kazi kwa bidii na hivyo kusababisha mapato hayo kufikia Sh 4.8 bilioni. 

“Mafanikio haya yametokana na juhudi za wafanyakazi. Mwaka jana niliwaomba wafanyakazi wafanye kazi kwa bidii, na wao walikubali. Imani yangu ni kwamba posho kwa wafanyakazi wangu zitaanza kulipwa baada ya bodi kupitisha ombi la kuwaongezea. Nafikiri tukiwaeleza vizuri bodi watatuelewa na hivyo wafanyakazi watapata kile tulichowaahidi,” amesema Profesa Museru. 

Mkurugenzi huyo amesema kwamba hospitali imepata mafanikio makubwa yakiwamo kuongeza huduma za afya kwa mfano kuanzishwa kwa huduma ya kusafisha figo, kuongeza wodi kwa wagonjwa wanaohitaji uangali maalumu, huduma za matumbo na kuboreshwa kwa mazingira ya kutolea huduma. 

Amesema hospitali hiyo inajitahidi kuongeza mapato zaidi ili iweze kulipia huduma za umeme, huduma za simu, ankra za maji pamoja na kudi za majengo.
“Sisi hatufanyi biashara bali tunatoa huduma kwa wagonjwa, tunapaswa kuongeza mapato ili kulipia huduma kutoka kwa washirika wetu akiwamo Tanesco, kulipia maji na huduma za simu,” amesema Kaimu Mkurugenzi huyo. 

Akizungumzia changamoto, Profesa Museru amesema sehemu zinazotumika kutoa huduma zinatakiwa kukarabatiwa. Amesema miundombinu inapaswa kukarabatiwa kwa  kuwa imekuwa ikichakaa kutokana na kuongezeka kwa wagonjwa hospitali hapo.
“ Majengo ya hospitali hayajakarabatiwa karibu miaka 20, hivyo tunapaswa kukarabati sasa,” amesema. 

Pia Profesa Museru amewapongeza wafanyakazi bora ambao wametunukiwa vyeti baada ya kuibuka kuwa wafanyakazi bora. 


Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Profesa Lawrence Museru akizungumza katika hafla ya kuwatunukia vyeti wafanyakazi bora 54. Hafla hiyo imefanyika katika hospitali hiyo. Wafanyakazi wa hospitali hiyo wakiwamo madaktari na wauguzi wakimsikiliza Profesa Museru Mwenyekiti wa TUGHE Tawi la Muhimbili, Mziwanda Chimwege akisoma risala kwa mgeni rasmi, Profesa Museru katika hafla ya kuwakabidhi vyeti wafanyakazi boraWafanyakazi wa hospitali hiyo wakimsikiliza Mwenyekiti wa TUGHE, Mziwanda Chimwege. 
William Chimwege wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Hospitali hiyo, akipokea cheti  kutoka kwa Mkurugenzi wa Uuguzi, Agness Mtawa baada ya kuchaguliwa kuwa mfanyakazi bora. Mkurugenzi wa hospitali hiyo, Profesa Lawrence Museru akimkabidhi cheti mfanyakazi wa Idara ya Ajira na Mafunzo, Farisha Jumanne baada ya kuchaguliwa kuwa mfanyakazi bora. Wafanyakazi wa Muhimbili wakiserebuka baada ya wafanyakazi bora kutunukiwa vyeti. Picha na John Stephen, Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH)  

No comments: