Wednesday, July 20, 2016

SERIKALI KUWEKA UTASHI WA KISIASA KATIKA MAPAMBANO DHIDI YA UTAPIAMLO- MAKAM WA RAIS.

Na Chalila Kibuda, Globu ya Jamii.

SERIKALI imesema kuwa itaweka utashi wa kisiasa katika kupambana dhidi ya utapiamlo kwa kuongeza elimu hususani katika maeneo ya vijijini.

Hayo ameyasema leo Makamu wa Rais, Samia Hassan Suluhu wakati wa uzinduzi wa ripoti ya Dunia iliyoandaliwa na Jukwa la Lishe Nchini (PANITA) , amesema kuwa suala la lishe likiwekewa utashi wa kisiasa litaweza kufanikiwa kutokana na jitihada ambazo zimeanza kuonekana kwa wadau.

Amesema serikali inatambua kuwa mojawapo ya malengo ya Baraza la Afya Duniani ni kutokomeza utapiamlo ifikapo mwaka 2025 na lengo hilo linaweza lisifikiwe kama tutaendelea kutekeleza mipango yetu kwa mazoea.

Makamu wa Rais Samia amesema kuwa serikali kwa kushirikiana na wadau wote kwa pamoja tuweze katika kutokomeza utapiamlo katika kufikia malengo ya Tanzania isiyo na Utapiamlo, Tanzania ya viwanda na yenye uchumi wa kati.

Amesema malengo kupambana na utapiamlo yatawezekana kwa kuendeleza jitihada za kuongeza bajeti za lishe,kuongeza virutubishi katika vyakula , kutumia vyema wataalam wa lishe na kuhakikisha utekelezwaji wa afua za lishe kwa ufanisi zaidi.

Makam wa Rais, Samia amesema kuwa ripoti imetilia mkazo suala la lishe kama msingi wa maendeleo hivyo kuzungumzia maendeleo inamaanisha afya,elimu ,ajira ,kuondoa umasikini na kuleta usawa.

Amesema suala la usawa limewaangalia kuwajengea uwezo wakina mama kutokana na akina mama kuwa walezi wa jamii ,wazalishaji wakubwa katika sekta ya kilimo lakini wanaume wanawajibu wa kushiriki katika suala hilo.

Nae Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia ,Wazee na Watoto , Ummy Mwalimu amesema kama wizara inatambua tatizo la lishe na kusema kwa kiwango tulichofikia lazima kipungue.

Makamu wa Rais, Samia Hassan Suluhu, Mkurugenzi wa Jukwaa la Lishe Tanzania (Panita), Tumaini Mikindo na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy  Mwalimu wakikata utepe kuashiria uzinduzi wa uzinduzi wa ripoti ya Dunia iliyoandaliwa na Jukwa la Lishe Nchini (PANITA) iliyozinduliwa jijini Dar es Salaam leo. 
Makamu wa Rais, Samia Hassan Suluhu akizungumza na wadau wa lishe katika uzinduzi wa ripoti ya lishe ya dunia katika uzinduzi uliofanyika jijini Dar es Salaam leo.
Mkurugenzi wa Jukwaa la Lishe Tanzania (Panita), Tumaini Mikindo akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo mara baada ya kuzindua ripoti ya lishe ya Dunia.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia ,Wazee na Watoto , Ummy Mwalimu akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kuzindua ripoti ya lishe ya dunia jijini Dar es Salaam leo.
Makamu wa Rais, Samia Suluhu akigawa ripoti ya lishe ya dunia iliyozinduliwa leo jijini Dar es Salaam.
Makamu wa Rais, Samia Hassan Suluhu akiwa katika picha ya pamoja na wadau wa lishe mara baada ya kuzindua ripoti ya afya jijini Dar es Salaam leo.

No comments: