Wednesday, July 27, 2016

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI, ENG. RAMO MAKANI AZINDUA MIRADI YA TANAPA CHAMWINO, DODOMA.

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Eng. Ramo Makani (kushoto) akizungumza na wananchi wa kijiji cha Ilangali Wilaya ya Chamwino Mkoani Dodoma jana muda mfupi kabla ya kuweka jiwe la msingi katika zahanati ya kijiji hicho. Mradi huo wa zahanati umefadhiliwa kwa ushirikiano wa TANAPA Tsh. Milioni 25, Mbunge wa Jimbo la Mtera (Livingstone Lusinde) Tsh. Milioni 14.3 na Wananchi wa kjiji hicho Tsh. Milioni 12. 
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Eng. Ramo Makani (kushoto) akizindua mradi wa bweni la wasichana katika shule ya Sekondari Maila iliyopo Chamwino, Dodoma jana, mradi huo umefadhiliwa kwa ushirikiano wa TANAPA kupitia Mradi wa Ujirani Mwema, Tsh. Milioni 115.83 na Wananchi wa Kata ya Manda Tsh. Milioni 33.72. Kulia ni Mbunge wa Jimbo la Mtera, Lingstone Lusinde.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Eng. Ramo Makani (kushoto) akimkabidhi Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, Vumilia Nyamoga (kulia) Hati ya Makabidhiano ya mradi wa bweni la wasichana katika shule ya Sekondari Maila iliyopo Chamwino, Dodoma jana, mradi huo umefadhiliwa kwa ushirikiano wa TANAPA kupitia Mradi wa Ujirani Mwema,  Tsh. Milioni 115.83 na Wananchi wa Kata ya Manda Tsh. Milioni 33.72. Watano kulia ni Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TANAPA, Witness Shoo.
 Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Hifadhi za Tanzania - TANAPA  ambaye pia Mkurugenzi wa Utawala na Utumishi wa Shirika hilo, Witness Shoo akitoa taarifa ya juu ya miradi miwili iliyofadhiliwa na Shirika hilo katika vijiji vya Ilangali na Manda. Alisema shirika hilo limechangia Tsh. Milioni 148.3 kupitia mradi wa Ujirani Mwema. 
 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Eng. Ramo Makani (wa pili kulia) akikagua vitanda vya mradi wa bweni la wasichana wa shule ya Sekondari Maila iliyopo Chamwino, Dodoma jana, mradi huo umefadhiliwa kwa ushirikiano wa TANAPA kupitia Mradi wa Ujirani Mwema, Tsh. Milioni 115.83 na Wananchi wa Kata ya Manda Tsh. Milioni 33.72. Kulia ni Mbunge wa Jimbo la Mtera, Lingstone Lusinde na Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino, Samuel Amon (wa tatu kulia).
 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Eng. Ramo Makani (wa tatu kulia) akiongoza msafara kukagua fensi ya bweni la wasichana katika shule ya Sekondari Maila muda mfupi kabla ya kuzinduliwa. Kulia ni Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TANAPA, Witness Shoo na Mbunge wa Jimbo la Mtera, Livingstone Lusinde (wanne kulia)
 Picha ya pamoja.
 Taswira ya jengo la Zahanati ya kijiji cha Ilangali lililofadhiliwa na TANAPA
 Taswira ya jengo la Bweni la Wasichana shule ya Sekondari Maila lililofadhiliwa na TANAPA.

Na Hamza Temba - WMU.
Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii imepanga kulipatia ufumbuzi tatizo la uvamizi wa Wanyamapori kwenye makazi ya watu wanaozunguka Hifadhi zenye Wanyamapori nchini kwa kuwashirikisha wananchi wa vijiji hivyo, kuwapatia mafunzo na silaha maalum za kujilinda na kufukuza wanyamapori hao wakati wa dharua.

Hayo yalibainishwa jana na Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Eng. Ramo Makani akizungumza na wananchi wa vijiji vya Manda na Ilangali Wilayani Chamwino Mkoa wa Dodoma wakati wa hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi na uzinduzi wa miradi iliyofadhiliwa na Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) kupitia Mradi wa Ujirani Mwema katika vijiji hivyo.

Akijibu kero iliyowasilishwa kwake na Mbunge wa Jimbo la Mtera, Livingstone Lusinge katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye vijiji hivyo kuhusu Wanyamapori wanaovamia maeneo ya vijiji vya jirani na Hifadhi ya Ruaha na kuharibu mazao ya wananchi, Eng. Makani alisema, changamoto hiyo inashuulikiwa kwa upana wake na kwamba Serikali inakuja na mpango wa kukabiliana nayo kwa kuwashirikisha wananchi wa vijiji husika.

Akizungumzia mpango huo alisema kuwa Serikali itaanzisha mafunzo maalum ya kujikinga na Wanyamapori kwa baadhi ya wananchi watakaoainishwa kwenye maeneo husika na kupewa silaha maalum kwa ajili ya kuwafukuza kabla ya kuleta madhara. Aliongeza kuwa Askari wa Wanyamapori waliopo pamoja na changamoto za kijiografia za baadhi ya maeneo hawatoshi kulinda maeneo yote ya vijijini hususani wakati wa dharua hivyo kwa kuwapa mafunzo na zana na kujilinda baadhi ya wananchi itasaidia katika kukabilina na tatizo hilo kwa wakati.

Katika hatua za maandalizi ya awali ya mpango huo, aliwaagiza viongozi wa vijiji vya Ilangali na Manda ambavyo vinayozunguka Hifadhi ya Taifa ya Ruaha kuanza kazi ya kutambua vijana wakakamavu, wenye elimu, uadilifu, uaminifu na maadili bora kuanzia watano hadi kumi kwa ajili ya kujiunga na mpango huo pale utakapokuwa tayari kuingia kwenye hatua ya utekelezaji.

Hapo awali akiweka jiwe la msingi kwenye mradi wa zahanati ya kijiji cha Ilangali na baadae kuzindua mradi wa bweni la wasichana shule ya Sekondari Maila  iliyofadhiliwa na TANAPA, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, Prof. Jumanne Maghembe, Naibu Waziri, Eng. Makani alisema kuwa misaada hiyo ni sehemu faida za uhifadhi ambayo wananchi wananufaika nayo kwa kushirikiana na Serikali katika uhifadhi. Aliwataka wananchi hao kuendelea kushirikiana na Serikali katika uhifadhi ili faida kama hizo ziendelee kupatikana kwa wingi kwa kuwa uhifadhi ukiimarika na wanyamapori wakaongezeka na utalii nao utakua na kuongeza mapato zaidi.

"Fedha zilizotumika katika Mradi huu tunaoushuhudia hapa leo ni sehemu ya faida za Uhifadhi, tunawaomba sana wananchi muendelee kuunga mkono juhudi za Serikali za kulinda Wanyamapori na kupiga vita ujangili, tuendelee kulinda chanzo cha fedha hizo, tukipata watalii wengi zaidi na fedha hizo zitaongezeka maradufu. Alisema Makani.

Akizungumzia miradi hiyo miwili, Kaimu Mkurugenzi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) ambaye pia ni Mkurugenzi wa Utawala na Utumishi wa Shirika hilo, Witness Shoo alisema kuwa shirika hilo limechangia Tsh. Milioni 148.3 katika miradi hiyo ya Ujirani Mwema. Aliongeza kuwa katika kipindi cha mwaka 1994 - 95 na 2014 - 15 Shirika hilo limechangia jumla ya Tsh. Bilioni 2 kwa vijiji vinavyozunguka Hifadhi ya Taifa ya Ruaha katika miradi ya sekta ya  ya elimu, maji, afya na uhifadhi kwa ujumla.

No comments: