Thursday, June 30, 2016

WAZIRI UMMY MWALIMU, MELINDA GATES WAYAPONGEZA MASHINDANO YA MAMA SHUJAA WA CHAKULA YANAYO ENDESHWA NA OXFAM TANZANIA


Mwenyekiti mwenza wa taasisi ya Bill and Melinda Gates ya Marekani Bi. Melinda Gates akiongea na wadau mbalimbali na kulipongeza shirika la Kimataifa la Oxfam Tanzania kwa kuendesha Shindano la Mama Shujaa wa Chakula ambalo lengo kubwa ni kuwawezesha wakulima wadogo wadogo wanawake kufanikiwa katika Kilimo cha chakula na umiliki wa ardhi.
Mkurugenzi Mkazi wa Oxfam Tanzania Jane Foster akitoa neno la utangulizi wakati wa sherehe hiyo.
Waziri wa Afya,Jinsia,Wazee na Watoto Mh. Ummy Mwalimu akilipongeza Shirika la Kimataifa la Oxfam Tanzania kwa kuendesha Shindano la Mama Shujaa wa Chakula ambalo linaonesha changamoto za wazalishaji wa chakula wadogo ikiwemo umiliki wa ardhi.
Mshereheshaji katika Hafla hiyo Maria Sarungi Tsehai akiendelea kutoa muongozo


Dkt. Eve Marie akizungumza kwa kina ni jinsi gani Serikali na Sekta binafsi zinaweza kuwekeza katika wakulima wadogo wadogo hasa wanawake ili kuongeza uzalishaji wa Chakula

Muwezeshaji kutoka Forum CC Faizal Issa akielezea namna wakulima ambavyo wanaweza kukabiliana na mabadiliko ya Tabianchi ambayo kwa sasa yanaathiri kwa kiasi kikubwa katika uzalishaji katika kilimo.

Mwanamuziki maarufu wa Muziki wa kizazi kipya Bongo Fleva Mwasiti akitumbuiza wakati wa Sherehe hizo

Mama Shujaa wa Chakula Anna Oloishuro akizungumzia jinsi mabadiliko ya tabianchi yanavyo athiri katika kilimo pia kuomba Benki mbalimbali nchini zisaidie wakulima kwa kuwakopesha na kuwapa riba ndogo.

Profesa Marjorie Mbilinyi akizungumzia swala zima za wazalishaji wa chakula wadogo kukosa masoko alisisitiza Sheria mbalimbali zifuatwe ili kukabilina na hali hiyo.


Mkurugenzi na Mwanzilishi wa Msichana Initiative Rebeca Gyumi akizungumzia tatizo la ajira kwa vijana Tanzania na kusisitiza ikiwa watawezeshwa katika mambo mbalimbali ikiwemo na umiliki wa Ardhi basi wataweza kufikia malengo yao.

Baadhi ya wageni wakiwa katika sherehe hizo wakifuatilia kwa makini mjadala uliokuwa ukiendelea fuatilia mjadala uliokuwa ukiendelea
Mwigizaji Maarufu wa Bongo Movie na Balozi wa Oxfam Tanzania Jacob Stephen JB akitaja majina washiriki 19 katika shindano la Mama Shujaa wa Chakula 2016 msimu wa tano
Aliyekuwa Mshiriki wa Shindano la Mama Shujaa wa Chakula Msimu wa nne na Rais wa wakulima wadogo wadogo wanawake Afrika Bi. Eva Daud Mageni akitoa neno la Shukurani kwa Mwenyekiti mwenza wa taasisi ya Bill and Melinda Gates ya Marekani na kumpa zawadi maalum ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wake katika kuendeleza jitihada za maendeleo Tanzania ikiwemo swala la Kilimo.
Mwenyekiti mwenza wa taasisi ya Bill and Melinda Gates ya Marekani akipokea zawadi maalumu kutoka kwa waliokuwa washiriki wa Shindano la Mama Shujaa wa Chakula Misimu iliyopita
Picha ya Pamoja ya Waziri wa Afya,Jinsia,Wazee na Watoto Mh. Ummy Mwalimu,Mwenyekiti mwenza wa taasisi ya Bill and Melinda Gates ya Marekani, Mkurugenzi Mkazi wa Oxfam Tanzania Jane Foster,Mabalozi wa Oxfam Tanzania pamoja na Baadhi ya Akina mama watakao Shiriki Shindano la Mama Shujaa wa Chakula 2016


Wadau kutoka sekta mbalimbali wakiwa katika Sherehe hiyo
Mkutano Maalum na waandishi wa Habari ukiendelea

Picha na Fredy Njeje


Waziri wa Afya, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu na mke wa tajiri namba moja duniani na mwenyekiti mwenza wa Bill and Melinda Gates Foundation, Melinda Gates kwa pamoja wamelipongeza Shirika la Oxfam kupitia kampeni yake ya Grow kwa kufanya Shindano la Mama Shujaa wa Chakula kama moja ya mbinu za kumkomboa mwanamke mnyonge kiuchumi.

Wawili hao waliyasema hayo kwenye mdahalo uliofanyika Juni 29 mwaka huu katika bustani ya Hoteli ya Serena jijini Dar ambapo walikuwa wageni waalikwa waliopata fursa ya kuzungumzia jinsi ya kumuwezesha kiuchumi mwanamke mzalishaji na namna ya kupambana na mabadiliko ya hali ya hewa.

Akizungumza kwenye mdahalo huo, Melinda Gates alisema kuwa yeye kupitia Bill and Melinda Gates Foundation wamelenga kusaidia nchi nyingi hasa za ukanda wa Afrika Mashariki kama Tanzania katika kubadilisha maisha yao kwa kutengeneza fursa za ajira na kuwasaidia vitendea kazi.

Aliongeza kuwa kwa nchi kama ya Tanzania ambayo asilimia 25 ya mapato yake yanatokana na kilimo, taasisi yao imejikita katika kuwawezesha wakulima wadogowadogo ambao hata hivyo huwezi kuwaacha wakina mama kwa kuwa ndiyo wanaotoa mchango mkubwa kwenye sekta hiyo.

Akizungumzia kuhusu Shindano la Mama Shujaa wa Chakula, Melinda Gates alitoa pongezi zake za dhati kwa shirika la Oxfam na kuongeza kuwa, ikiwa nchi za Kiafrika hususan Tanzania itataka kupiga hatua lazima iwawezeshe kiuchumi wanawake kwa kuwa wao ndiyo wenye uwezo wa kubadilisha maisha yao na hilo ndiyo jambo muhimu zaidi. 


Naye Waziri wa Afya, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu ambaye alikuwa ni mgeni rasmi kwenye mdahalo huo alisema kuwa; kwa kipindi kirefu amekuwa mfuatiliaji wa mashindano hayo na kuahidi kuwa sera ya serikali ya awamu ya tano ni kuongeza vipaumbele kwa mwanamke kwa kutoa mianya kwa taasisi zinazomsaidia mwanamke ikiwemo shirika la Oxfam kupitia shughuli zake hasas shindano la mama shujaa wa chakula. “Nikiri tu kuwa nimekuwa mfuatiliaji mzuri sana wa shindano hili tangu zamani, naahidi kuwapa ushirikiano mkubwa kwenu kwa kila jambo kwa kuwa mnaisaidia sana serikali,” alisema Ummy.

Aidha mdahalo huo pia ulioongozwa na mwanaharakati, Maria Sarungi Tsehai ulihudhuriwa na wanaharakati wengine wa masuala ya jinsia akiwemo Mkurugenzi wa Msichana Initative, Rebecca Gyumi, Mwanaharakati wa Mtandao wa Masuala ya Kijinsia, Marjorie Mbilinyi, Mwezeshaji kutoka Forum CC, Faizal Issa na Mshindi wa Shindano la Mama Shujaa wa Chakula 2011, Anna Oloishuro.

No comments: