Tuesday, April 26, 2016

TIMU YA BUNGE SPORTS CLUB KUSHUKA DIMBANI LEO DHIDI YA TIMU YA BARAZA LA WAWAKILISHI ZANZIBAR

Timu ya Mpira wa miguu ya Bunge la Jamhuri ya Muungano la Tanzania, Bunge Sports Club jioni ya leo kinatarajiwa kushuka dimbani kucheza mchezo maalum na wa kwanza dhidi ya timu ya Baraza la Wawakilishi la Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, mchezoutakaochezwa uwanja wa Amaan, Unguja.


Tayari asubuhi ya leo kikosi hicho cha timu ya Bunge kimefanya mazoezi ya mwisho kujiandaa na mchezo huo wa jioni ambao unatarajia kuchezwa majira ya saa 12:45 Jioni katika uwanja wa Amaani. Kikosi hicho kinachonolewa na Kocha wa timu hiyo ambaye pia Mbunge Jimbo la Kilolo mkoani Iringa, Mh. Venance Mwamotto amebainisha kuwa lengo la mchezo huo ni kiuimalisha Muungano ambapo pia michezo ni afya hivyo mchezo utakuwa ni wa ushindani na wa kuvutia kwa pande zote mbili.

“Tunawaomba wabunge wote kutuunga mkono katika mchezo huu kwani tmu imejindaa vya kutosha kuhakikisha tunashinda wetu huu wa leo Aprili 26 katika uwanja wa Amaan karibuni watu wote kutushuhudia tutakavyoonyesha uwezo wa hali ya juu katika michezo” alieleza Mh. Mwamotto.

Naye Mbunge wa Korogwe Vijijini (CCM), Mh. Steven Ngonyani ‘Maji Marefu’ ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ufundi wa timu hiyo ya Bunge amewaomba wachezaji wa timu hiyo kuhakikisha wanapiga hatua kwani timu ni nzuri na ina hali ya ushindi kwa pande zote hivyo anahakika na kuibuka na ushindi kwa mchezo wa leo.

Kwa upande wake Mbunge wa Nzega Vijijini ambaye pia ni Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mh. Dkt. Hamisi Kigwangalla ambaye ni Mwenyekiti wa timu ya Bunge amewataka wabunge wote wanaounda timu hiyo kuzingatia maelekezo ya Kocha pamoja na kuzingatia taratibu za mchezo wa soka ilikuweza kupata ushindi mnono.

Kwa upande wa Kapteni mpya wa timu hiyo, ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Mbinga Mjini, Mh. Sixtus Mapunda amesema kikosi cha timu yake kimejiandaa vya kutosha na kiko kamili kwa mchezo huo wa jioni ya leo huku akiahidi ushindi mkubwa.

Mchezo huo wa Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar ni maalum kwa ajili ya maadhimisho ya Muungano wa Nchi ya Jamhuri ya Tanganyika Na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar ambapo jioni ya leo viongozi mbalimbali watajumuika kushuhudia mchezo maalum.

Kikosi cha Bunge chenye wachezaji zaidi ya 19 kimejiandaa vya kutosha katika kuakikisha inapata ushindi mnono ambapo kimepiga kambi visiwni hapa kwa siku kadhaa hivyo mchezo huo utakuwa ni wa ushindani kwa pande zote mbili licha ya timu ya Baraza la Wawakilishi ambayo imejaa vijana wengi yenyewe ikiwa imejificha katika kambi yao nje ya mji wa Unguja.

Aidha, mbali na mchezo huo, pia kutakuwa na michezo mingine ikiwemo mchezo wa Ligi ya Zanzibar pamoja na mchezo maalum ambapo Wekundu wa Msimbazi Simba Sc ikitarajiwa kushuka dimbani kucheza na moja ya timu ya Visiwani hapa mchezo ambao ni wa kirafiki katika kunogesha Muungano huo.
Kapteni mpya wa timu ya Bunge ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Mbinga Mjini, Mh. Sixtus Mapunda akifanya mazoezi ya mwisho mwisho asubuhi ya leo katika uwanja wa Amaan, Unguja
Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Yusuf Masauni akiwa katika mazoezi hayo leo uwanja wa Amaan
Mbunge wa Mbulu Vijijini , Mh.Flatei Massay akifanya mazoezi katika kujiandaa na mchezo huo wa leo jioni
Mbunge wa jimbo la Sengerema, William Ngeleja ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa timu hiyo akiwa katika mazoezi hayo
Kikosi cha Bunge kikipata maelezo ya kina kutoka kwa kocha wao, Mh. Mwamotto
Kocha wa Bunge Mh. Mwamotto akitoa maelekezo ya namna ya kumiliki mpira timu iwapo uwanjani.
Benchi la ufundi la timu ya Bunge likifuatilia mazoezi hayo ya mwisho leo asubuhi 
Mbunge wa Nzega Vijini ambaye pia ni Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mh. Dkt. Hamisi Kigwangalla ambaye ni Mwenyekiti wa timu hiyo ya Bunge (kushoto) akiwa katika mazoezi ya mwisho mwisho dhidi ya mchezo wa leo jioni.

Mbunge wa Mbulu Vijijini , Mh.Flatei Massay akiwa katika mazoezi pamoja na Mbunge wa jimbo la Sengerema, William Ngeleja (juu) katika mazoezi hayo.
Kocha akitoa maelezo ya mwisho Waziri wa Kilimo, Mfugo na Uvuvi Mh. Mwigulu Nchemba akionyesha umahiri wa kumiliki mpira wakati wa mazoezi hayo ya asubuhi ya leo tayari kujiandaa na mchezo wa hapo jioni


Timu ya Bunge ikitoka uwanjani mara baada ya kumaliza kwa mazoezi yao asubuhi hii
Waziri wa Kilimo,Mifugo na Uvuvi Mh.Mwigulu Nchemba akisalimiana na wachezaji wenzake wa timu ya Bunge wakati alipoungana nao. Mwigulu ni miongoni mwa wachezaji wa Bunge wa kutegemewa ambapo aliweza kuunhana na kikosi hicho na kuongeza hali ya mchezo kwa hapo jioni.
Kikosi cha timu ya Bunge ambacho kitashuka dimbani jioni ya leo kimejiandaa vya kutosha kwa mujibu wa kocha wa timu hiyo ambapo amebainisha kuwa, wachezaji wake wote wameshaandaliwa kisaikolojia na kimchezo hivyo wanatarajia ushindi wa kishindo. (Picha zote na Andrew Chale -Zanzibar).

No comments: