Monday, April 4, 2016

Kamati ya Afya ya Bunge Yaitembelea Hospitali ya Muhimbili Leo

Na John Stephen

Kamati ya Afya ya Bunge leo imeitembelea Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) kwa ajili ya kukagua huduma  mbalimbali za afya zinazotolewa na hospitali hiyo.


Ziara hiyo imeongozwa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Peter Joseph Serukamba  akiwamo Mussa Azzan Zungu na wabunge wengine wa kamati hiyo.

Wabunge hao wametembelea Idara ya Magonjwa ya Dharura na Ajali (EMD), Idara ya Magonjwa ya Akili, Idara ya Mionzi na Wodi ya Mwaisela na chumba cha kuchakacha gesi ambayo inatumika wakati wa kutoa tiba kwa wagonjwa mbalimbali.


Daktari wa magonjwa ya Dharura na Ajali, Upendo Ndara amewaeleza wabunge hao jinsi madaktari na wauguzi wanavyowahudumia wagonjwa wanaofikishwa kwenye idara hiyo, changamoto na jinsi wanavyofanikiwa kuokoa maisha ya wagonjwa wa ajali na wagonjwa wengine.

Pia, Dk Upendo ameelezea juhudi kubwa zinazofanywa na Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) katika kupanua jengo la idara hiyo ili kutoa huduma bora za matibabu kwa wagonjwa.

Naye Mkuu wa Idara ya Magonjwa ya Afya ya Akili, Frank Massawe amewaeleza wabunge mafanikio yaliopatikana baada ya wagonjwa wa akili kupatiwa matibabu na changamoto zinazoikabili hospitali hiyo.
Daktari wa Idara ya Magonjwa ya Dharura na Ajali, Upendo Ndara akiwaongoza wabunge kuona huduma mbalimbali zinazotolewa na madaktari na wauguzi wa idara hiyo Leo.
Dk. Upendo Ndara wa Idara ya Magonjwa ya Dharura na Ajali akiwaeleza wabunge wa Kamati ya Afya jinsi idara hiyo inavyowahudumia wagonjwa wa dharura na ajali wanaofikishwa hapo kwa ajili ya kupatiwa matibabu.
Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Hamis Kigwangallah akifafanua jambo kwa Kamati ya Bunge ambayo imeitembelea leo hospitali hiyo.
Dk Upendo Ndara wa Idara ya Magonjwa ya Dharura na Ajali akiewaeleza wabunge wa Kamati ya Afya juu ya upanuzi wa jengo la kuwahudumia wagonjwa wa dharura na ajali kwenye hospitali hiyo.
Mkuu wa Idara ya Wagonjwa wa Afya Akili, Dk Frank Massawe akiwaeleza wabunge wa Kamati ya Afya jinsi idara hiyo inavyotoa tiba kwa wagonjwa wa akili.
Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Profesa, Lawrence Museru akifafanua jambo kwa Kamati ya Bunge ya Afya kuhusu huduma zinazotolewa kwa wagonjwa wa akili.
Mkuu wa Idara ya Mionzi, Dk Flora Lwakatare (mwenye koti) akiwaeleza wabunge wa Kamati ya Afya jinsi mashine ya CT- SCAN inavyochukua vipimo mbalimbali kwa wagonjwa. Dk Lwakatare amewaeleza wabunge hao kwamba mashine hiyo ina uwezo mkubwa wa kugundua matatizo ya wagonjwa.

No comments: