Friday, March 11, 2016

WAKALA WA MAJENGO TANZANIA YAIPA MKATABA YONO AUCTION MART WA KUKUSANYA MADENI NCHINI

Na Dotto Mwaibale

WAKALA  wa Majengo Tanzania (TBA), umecharuka kwa kuingia mkataba na Kampuni ya Udalali ya Yono Auction Mart & Co. Ltd ili kusaidia kukusanya madeni ya wadaiwa sugu ambao walikopa nyumba.

Wakati huo huo mwakilishi wa kampuni hiyo ya udalali ya Yono Auction Mart & Co. Ltd, Scollastica Kevela ametoa siku tatu kwa wadaiwa wote wa TBA kuhakikisha wanalipa fedha hizo kabla ya kufikiwa na kampuni hiyo ambayo Jumatano ya Machi 16 mwaka huu itaanza rasmi kazi ya kuwaondoa katika nyumba za wakala huo watumishi wote wanaodaiwa kwa kufuata sheria kama inavyoelekeza.

Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Dar es Salaam leo wakati wa kutiliana saini na kampuni hiyo ya udalali kwa ajili ya kukusanya fedha kutoka kwa wadeni wa wakala huo  Mtendaji Mkuu wa TBA ,  Elius Mwakalinga alisema wamefia hatua hiyo baada ya kuona wadaiwa wao ambao wengi wao ni kutoka sekta za serikali kushindwa kulipa fedha hizo.

"Tumeingia mkataba na Kampuni ya Yono Auction Mart baada ya kushinda zabuni ambayo tulitangaza Februari 23,2016 na sasa kazi yote ya ukusanyaji wa fedha hizo itafanywa na kampuni hiyo" alisema Mwakalinga.

Mwakalinga alisema fedha nyingi za wakala huo zipo mikononi mwa wadaiwa wao ambapo kwa mkoa wa Dar es Salaam na Dodoma ni shilingi.Bilioni 6 na kwa waliokopa ni sh.milioni 800 huku fedha zinazodaiwa kwa ajili ya kutoa ushauri mbalimbali wa ujenzi ni sh.bilioni 6.95.

Mwakilishi wa kampuni  ya Yono Auction Mart & Co. Ltd, Scollastica Kevela alisema wametoa siku tatu kwa wadaiwa wote kuhakikisha wanalipa fedha hizo vinginevyo watafikiwa na kampuni hiyo ambayo imepanga rasmi kupita kila nyumba inayodaiwa na kuwa kila muhusika atatakiwa kuilipa kampuni hiyo asilimia tano ya fedha anazodaiwa na TBA.
 Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) ,  Arch. Elius Mwakalinga (kushoto), akikabidhiana hati ya mkataba na Mwakilishi wa Kampuni ya Udalali ya Yono Auction Mart & Co. Ltd, Scollastica Kevela Dar es Salaam leo asubuhi, baada ya kampuni hiyo kushinda zabuni ya kukusanya madeni ya TBA kuanzia leo.
 Taswira meza kuu katika mkutano huo.
 Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) , Arch Elius Mwakalinga (katikati), akizungumza katika mkutano huo kabla ya kutiliana saini na kampuni ya Yono. Kushoto Ofisa wa Idara ya Manunuzi, Mariam Kazoba.
 Ofisa wa Idara ya Manunuzi wa TBA, Mariam Kazoba, akitoa ufafanuzi mbalimbali katika mkutano huo.
 Mwakilishi wa Kampuni ya Udalali ya Yono Auction Mart & Co. Ltd, Scollastica Kevela (kulia), akizungumza katika mkutano huo ambapo alisema Yono wamejipanga kuwafikia wadaiwa wote wa TBA.
 Mkataba akisainiwa kwa pande zote.
(Imeandaliwa na mtandao wa www. habari za jamii.com)

No comments: