Thursday, March 3, 2016

MRADI WA KUTOKOMEZA VIFO VYA WAJAWAZITO NA WATOTO WACHANGA WAZINDULIWA

 Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk.Hamis Kigwangalla(katikati)akielekezwa jambo na Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano na Uhusiano wa Vodacom Tanzania,Rosalynn Mworia(kulia)wakati alipowasili katika hafla ya  uzinduzi wa Mradi wa Moyo awamu ya Pili unaofadhiliwa na Vodacom Foundation iliyofanyika wilayani Sengerema mkoani Mwanza juzi,kushoto Mkurugenzi mtendaji wa kampuni hiyo,Ian Ferrao.
  Mwenyekiti wa Bodi ya Vodacom nchini, Balozi Mwanaidi Maajar akihutubia katika  uzinduzi wa Mradi wa Moyo awamu ya Pili unaofadhiliwa na mtandao wa simu nchini Vodacom katika hafla ya uzinduzi iliyofanyika wilayani Sengerema mkoani Mwanza juzi.
Mkurugenzi wa Vodacom Tanzania, Ian Ferrao akihutubia katika  uzinduzi wa Mradi wa Moyo awamu ya Pili unaofadhiliwa na mtandao wa simu nchini Vodacom katika hafla ya uzinduzi iliyofanyika wilayani Sengerema mkoani Mwanza juzi.
 Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk.Hamis Kigwangalla akihutubia wakati wa hafla ya  uzinduzi wa Mradi wa Moyo awamu ya Pili unaofadhiliwa na Vodacom Foundation iliyofanyika wilayani Sengerema mkoani Mwanza juzi.
 Mkurugenzi wa Vodacom Tanzania, Ian Ferrao akimkaribisha Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk.Hamis Kigwangalla katika uzinduzi wa Moyo awamu ya Pili unaofadhiliwa na Vodacom Foundation uliofanyika juzi katika Wilaya ya Sengerema mkoani Mwanza juzi.
 Mkazi wa Sengerema mkoani Mwanza, Lawrencia John akimuonyesha Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk.Hamis Kigwangalla,Mwenyekiti wa Bodi ya Vodacom Foundation, Balozi Mwanaid Sinare Maajar, Mkurugenzi wa Vodacom nchini, Ian Ferrao(kulia) mtoto wake Mwalu John aliyejifungua baada ya kupata msaada wa mradi wa Moyo unaofadhiliwa na Vodacom Foundation jana katika uzinduzi wa Mradi huo awamu ya pili mkoani humo.
Kaimu Mkurugenzi wa USAID nchini, Bethany Haberer akisoma hotuba  wakati wa hafla ya uzinduzi wa Mradi wa Moyo awamu ya Pili unaofadhiliwa na Vodacom Foundation iliyofanyika wilayani Sengerema mkoani Mwanza juzi.

NAIBU Waziri wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dk. Hamis Kigwangala amezindua mradi wa kutokomeza vifo vya akina mama wajawazito na watoto wachanga nchini,Mradi huo umezinduliwa jana wilayani Sengerema mkoani Mwanza ambapo unafadhiliwa na taasisi ya Vodacom Foundation kwa kushirikiana na mashirika ya kimataifa ya USAID,Path Finder na Touch Foundation.
Mradi huu ambao unajulikana kama”MOYO”awamu ya pili umelenga kuunga mkono jitihada za serikali za kuboresha sekta ya afya nchini na adhma ya kutokomeza vifo vya akina mama wajawazito na watoto wachanga nchini.
Akiongea wakati wa hafla ya uzinduzi iliyofanyika mjini Sengerema Naibu Waziri wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dk. Hamis Kigwangala amesema kuwa mradi huu unaenda sambamba na malengo ya serikali ambayo imejipanga kuhakikisha matukio ya vifo vya akina mama wajawazito na watoto wachanga vinavyojitokeza wakati wa kujifungua kutokana na ukosefu wa huduma za matibabu vinatokomezwa.

“Katika kukabiliana na tatizo hili ambalo limetukutanisha  hapa siku ya leo na kuboresha huduma za matibabu nchini,serikali inatarajia kujenga wodi za akina mama wajawazito katika vituo vyote vya Afya nchini vilivyopo vijijini na mijini hivyo nawapongeza kwa kuiunga mkono serikali na natoa wito kwa wananchi wote kuelewa jitihada hizi na kuvitumia vituo hivi na huduma hizi ili kufanikisha lengo lililokusudiwa”.Alisema Dk. Hamis Kigwangala.

Mkurugenzi mtendaji wa Vodacom Tanzania, Ian Ferrao amesema tangu mradi wa MOYO awamu ya kwanza ulianza kutekelezwa mwaka 2009 na umefanikiwa kuandikisha wanawake zaidi ya elfu 16,000 katika vituo vya afya, na kuokoa maisha ya akina mama wajawazito na Watoto zaidi ya 450.
Alisema zipo baadhi ya changamoto kadhaa za baadhi ya akina mama wajawazito kutojifungua katika vituo vya Afya, ambapo licha ya changamoto hizo  mradi huo umewezesha mafunzo  kwa wahudumu wa Afya wa ngazi ya Jamii wanaopita kila kaya kutoa elimu, ili kubadili mitazamo hasi ya baadhi ya akina mama kutofika kwenye vituo vya afya kupatiwa huduma za uzazi.

“Kupitia mradi huu ambao pia umelenga kurejesha fadhila kwa wateja wetu tutagharamia usafiri wa akina mama wajawazito kupitia huduma ya M-Pesa kama ambavyo ilikuwa kwenye awamu ya kwanza ya mradi ili waweze kufika kwenye vituo vya afya kupata matibabu haraka pindi patakapohitajika msaada “,Alisema.

Mwenyekiti wa Bodi ya Vodacom Foundation, Balozi Mwanaidi Sinare Maajar, amesema pamoja na mafanikio  ya kiafya  yaliyopatikana kwa kukabiliana na ugonjwa wa Fistula na huduma ya ujumbe mfupi wa maneno ya kuelimisha akina mama masuala ya uzazi kupitia mradi wa WAZAZI NIPENDENI kusaidia akina mama wengi, vilevile zoezi hilo limekuwa likiviwezesha vikundi vya kuweka na kukopa vya Wanawake na kuwapatia mafunzo ya kuwawezesha kijikwamua  kiuchumi.

“Kupitia matumizi ya teknolojia ya huduma za simu za mkononi, kampuni imeweza kuboresha maisha ya wananchi.Nawapongeza wadau wote ambao tumekuwa tukishirikiana nao hasa Shirika la Msaada la watu wa Marekani (USAID).

Mkazi wa Sengerema Mwanza Lawrencia John, ambaye ni mmoja wa wanawake walionufaika  aliupongeza mradi huu na kusema ulimsaidia alipokuwa kwenye hali ya uchungu wakati wa kujifungua mtoto wake wa kwanza. Alipopiga simu aliweza kusaidiwa mara moja na amejifungua salama kabisa na anatoa wito kwa wadau wengine waweze kujitokeza kunufaika na huduma hii.

No comments: