Thursday, March 31, 2016

MAKAMU WA PILI WA RAIS BALOZI SEIF ALI IDD AKARIBISHWA OFISINI KWAKE

 
 Watendaji wa Taasisi zilizochini ya Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar wakimpokea na kumkaribisha kuanza kazi Ofisini kwake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi baada ya kuteuliwa tena na Rais wa Zanzibar kuendelea kushika wadhifa huo katika kipindi cha Pili cha Awamu ya Saba.
 Katibu wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Abdullah Ali Abdullah { Kitole } aliyeinama akinong’onezana kitu na Kaimu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Nd. Ahmad Kassim kwenye hafla ya kupokea Balozi Seif kuanza rasmi majukumu yake Vuga Mjini Zanzibar.
  Kaimu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Nd. Ahmad Kassim akimpongeza Balozi Seif kutokana na juhudi zake zilizopelekea watendaji wa ofisi yake kupata mafanikio makubwa ndani ya kipindi cha uongozi wake wa miaka mitano iliyopita.
 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif akiwashukuru watendaji wa Taasisi zilizo chini ya Ofisi yake baada ya kufanyakazi pamoja atika kipindi cha miaka mitano iliyopita.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema Watendaji wa Taasisi za Umma Nchini wanapaswa kuwa makini katika kusimamia ipasavyo matumizi ya fedha kwenye Taasisi zao ili kuipa nguvu Serikali kuu kuvuka vyema katika kipindi hichi cha mpito.

Alitahadharisha kwamba kipindi hichi hali ya fedha si nzuri kutokana  na mambo mengi yaliyofanywa katika kipindi kifupi kilichopita ikiwemo suala la uchaguzi Mkuu ambalo limelazimika kutumia fedha nyingi.

Balozi Seif Ali Iddi alitoa kauli hiyo wakati akizungumza na Wawakilishi wa watendaji wa Taasisi zilizo chini ya Ofisi yake walipompokea rasmi kuingia ofisini kwake na kuanza kazi mara baada ya kuteuliwa tena na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dr. Ali Mohammed Shein kushika wadhifa huo katika kipindi chengine cha miaka mitano ijayo.

Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imejipanga kuendesha Taasisi zake za Umma kwa kutumia fedha inazokusanya kupitia vianzio vyake mbali mbali chini ya usimamizi wa watendaji watakaoonyesha uadilifu kwenye usimamizi huo.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alielezea kuchukiwa kwake na baadhi ya watendaji wa Umma wenye tabia mbaya ya kuwekeana chuki katika utekelezaji wa majukumu yao yanayowakabili ya kila siku.

Balozi Seif alisema tabia hiyo potofu  inayolaaniwa hata katika imani  na Vitabu vya  Kidini ikiachiliwa kuendelea hatma yake inaweza kuzaa uadui utakaoleta hasara kubwa hapo baadae.

Aliwapongeza na kuwashukuru Viongozi pamoja na watendaji wa Taasisi zilizo chini ya Ofisi yake kwa kazi kubwa waliyoifanya iliyomuwezesha kutekeleza majuku yake ya ufanisi mkubwa ndani ya kipindi cha miaka mitano ya uongozi wake.

Balozi Seif aliwanasihi Viongozi na watendaji hao kuendelea kushirikiana na kushikamana kwa kufanya kazi kama ndugu wamoja ili kazi ya Utumishi waliokabidhiwa na Taifa ifikie malengo yaliyokusudiwa.

Alisema zipo kasoro, changamoto na hata mikwaruzano iliyojitokeza na kupelekea kukoseana baina ya baadhi ya watendaji na Viongozi hao akiwemo na yeye pia ndani ya kipindi kilichopita cha miaka mitano. Hivyo njia pekee ya kuzishinda changamoto na kasoro hizo ni kusameheana ili kufuta kasoro hizo.

Mapema Kaimu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Nd. Ahmad Kassim kwa niaba ya watendaji wa Ofisi hiyo amempongeza Balozi Seif kwa kuteuliwa tena kushika wadhifa huo. 

Nd. Ahmad alisema ndoto na dua za Viongozi na Watendaji wa Taasisi za Ofisi hiyo zimesibu kwa Mwenyezi Muungu aliyempa ilham Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dr. Ali Mohammed Shein kumteua tena Balozi Seif kuendelea kuwa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar.

Alisema ahadi waliobeba Viongozi na Watendaji wa Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ni kushirikiana nae bega kwa bega kadri ya uwezo wao kiutendaji ili kufanikisha majukumu yao kwa upeo mkubwa zaidi.

 Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
31/3/2016

No comments: