Monday, February 1, 2016

TANZANIA KUWACHUKULIA HATUA ZA KINIDHAMU NA KISHERIA MAHAKIMU 508 WALIOTEKELEZA MAJUKUMU YAO CHINI YA KIWANGO. ASEMA JAJI MKUU MHE. MOHAMED CHANDE OTHMAN



 Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Mohamed  Chande Othman akizungumza wa waandishi wa Habari kuhusu kuanza kwa Mwaka wa Sheria 2016, Wiki ya Sheria na Utendaji wa Mahakama ya Tanzania kwa mwaka 2016. Wengine Kushoto ni Jaji Mkuu wa Zanzibar Mhe. Omary Othman Makungu (Kushoto) na Jaji Kiongozi Mhe. Shaaban Lila (kulia).
 Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Mohamed Chande Othman (kushoto) akiwa ameambatana na Jaji Mkuu wa Zanzibar Mhe. Omary Othman Makungu (Katikati) na Jaji Kiongozi Mhe. Shaaban Lila (kulia) wakielekea kwenye mabanda ya Maonesho ya Wiki ya Sheria  kwa mwaka 2016  katika viwanja vya Mnazi Mmoja ambapo kilele cha Wiki hiyo kitakuwa Februari 4 2016 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli anatarajiwa kuwa mgeni rasmi.
 Baadhi ya Wananchi wakipata huduma katika mabanda ya maonesho wakato wa Maadhimisho ya Wiki ya Sheria.
Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Mohamed Chande Othman akitembelea banda la maonesho la Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka Wakati wa Maadhimisho ya Wiki ya Sheria nchini leo viwanja vya Mnazi mmoja.

Na Aron Msigwa –  MAELEZO
Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Mohamed Chande Othman amesema kuwa Mahakama ya Tanzania itawachukulia hatua za kinidhamu na za kisheria Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo,Wilaya na wale wa Mahakama za Hakimu Mkazi wapato 508 kote nchini waliotekeleza majukumu yao chini ya kiwango na kushindwa kutimiza wajibu wa Mahakama wa Utoaji wa Huduma Bora kwa wananchi katika mwaka wa Sheria wa 2015/2016.

Akizungumza na waandishi wa Habari leo jijini Dar es salaam alipokua akitoa ufafanuzi kuhusu  kuanza kwa mwaka mpya wa Sheria wa 2016 na Maadhimisho ya Wiki ya Sheria ambayo kilele chake kitakua Januari 4,2016 Mhe.Othman amesema  kuwa kwa mujibu wa taratibu za uendeshaji wa Mahakama na upimaji wa viwango vya utendaji kazi vilivyowekwa, Mahakimu hao wa Mahakama za wilaya na Hakimu Mkazi 121 na 387 wa Mahakama za Mwanzo watatakiwa  kutoa maelezo ndani ya siku 7 juu ya sababu zilizowafanya washindwe kutimiza lengo lililowekwa la kushughulikia mashauri 260 kila mmoja.
Amesema watakaothibitika  kamati za nidhamu na maadili za kila wilaya na Mikoa ambazo ni Kamati ndogo za Tume ya Utumishi wa Mahakama zitawafungulia kesi za kinidhamu ndani ya siku 21.
“Wale watakaobainika watakumbwa na adhabu ya kupewa Onyo, kushushwa vyeo na kufukuzwa kazi ili iwe fundisho kwa wengine, ninajua wapo baadhi ambao waliajiliwa katikati ya mwaka, wengine kwenda mafunzo ya vitendo vyuoni, wajawazito na baadhi vituo vyao kuwa na kesi chini ya 260 kwa mwaka” Amesisitiza.
Aidha, katika hatua hiyo amewapongeza Mahakimu waliofanya vizuri katika utendaji wao wakiwemo 14 walioshughulikia mashauri zaidi ya 700 kila mmoja, Mahakimu 50 walioamua kesi zaidi ya 500 kila mmoja baadhi wakitokea wilaya ya Mkuranga, Rufiji  na Bukoba mjini na wengine wawili kutoka Dar es salaam walioamua kesi zaidi ya 900 kila mmoja na  kuvuka lengo la utendaji lililowekwa la kushughulikia mashauri 260 kwa mwaka.

Akitoa tathmini ya utendaji wa Mahakama kwa mwaka wa sheria uliopita amesema kuwa Mahakama ya Tanzania ina Mahakama za Hakimu Mkazi kila Mkoa na Mahakama za Wilaya 111 katika wilaya za Kiserikali 133 pamoja na Mahakama za Mwanzo ambazo hupokea asilimia 93 ya mashauri yanayofunguliwa kote nchini.
 Amesema mwaka 2015 Mahakama zote nchini zilipokea jumla ya mashauri 206,115, kati ya hayo mashauri 220,815 yaliamuliwa kukiwa na ziada ya mashauri 14700 jambo linaloonyesha kuwa Mahakama zinapokea mashauri na kuyashughulikia kwa kasi inayoridhisha huku mashauri yanayosababisha mrundikano ni yale yaliyo nje ya idadi iliyopangwa.

Ameongeza kuwa katika katika kipindi cha mwaka huo wa 2015 Mahakama za Mwanzo zilipokea mashauri 141,025 ambapo kati ya hayo Mashauri 149,757 yalishughulikiwa huku idadi ya Mahakimu walioshughulikia mashauri hayo ni 1240.
“Ukiangalia mwenendo wa ufunguaji wa mashauri yote kote nchini hasa Tanzania Bara utagundua kuwa Mahakama za Mwanzo, Wilaya na zile za Hakimu Mkazi  zinapokea mashauri mengi kwa asilimia 93 ,katika kila mashauri 4 yanayofunguliwa nchini 3 yako mahakama za mwanzo ambako wananchi wengi wanatafuta ufumbuzi wa kesi zao lazima tuweke mkazo” Amesema Jaji Mkuu Mhe.Othman.
Kuhusu kuanza kwa mwaka mpya wa Sheria mwaka 2016 amesema Mahakama inauanza chini ya Kauli Mbiu Isemayo “Huduma Bora kwa Wananchi ni Wajibu wa Mahakama na Wadau wake”  ikiwa na kesi 20,431 ikilinganishwa na 34,126 ilizoanza nazo mwaka 2015 na kuongeza kuwa licha ya changamoto zinazoikabili Mahakama ya Tanzania mkakati uliopo ni kupunguza idadi hiyo hadi kufikia 0 kwa kila mwanzo wa mwaka wa sheria.

Akitoa ufafanuzi kuhusu upatikanaji wa Nakala za hukumu amesema Serikali inaendelea kuijengea uwezo wa kifedha Mahakama wa kuajiri wachapaji wa nakala wengi zaidi ili Nakala za Hukumu za Kesi ziweze kupatikana pindi tu kesi zinapomalizika katika mahakama zote nchini tofauti na ilivyo sasa ambapo hupatikana Mahakama Kuu na Mahakama za Rufani

Aidha, amesema Mahakama inaendelea kuboresha miundombinu yake ikiwemo majengo na ujenzi wa mahakama mpya katika maeneo yasiyo na huduma hiyo katika mwaka 2016. “ Hivi sasa tuna wilaya 23 hazina Majengo ya Mahakama za wilaya, kwenye baadhi ya maeneo kesi zinasikiliziwa Ofisini kwa Hakimu wakati ilitakiwa ziwe kwenye jengo lenye ukumbi wa wazi,tumejiandaa kwa michoro ya majengo kwa mahakama zote ili tuanze kujenga kwa gharama nafuu”  
Mhe. Othman ametoa wito kwa wananchi kutosita kuitumia Mahakama ya Tanzania katika kupata ushauri wa kisheria kupitia wataalamu wake, kuhudhuria maonesho mbalimbali ya kisheria yanayofanyika nchini huku akitoa angalizo kwa baadhi ya watu wanaochangia kuwepo kwa mrundikano wa kesi kwa kufungua kesi za madai au kupeleka mashauri Mahakamani kama sehemu ya maegesho ya masuala yao.

“Baadhi ya watu wamekuwa wakipeleka kesi Mahakamani kama sehemu ya maegesho, huzifungua kisha hushindwa kujitokeza Mahakamani hizi ni tofauti na zile zenye vipengele vingi ndani ya kesi moja au zile ambazo mashahidi wake wamehama kutoka eneo moja kwenda linguine, hizi nawahakikishia tutazifuta ili kupunguza mrundikano wa kesi kwenye Mahakama zetu” Amesisitiza Mhe. Othman.



No comments: