Saturday, January 16, 2016

SERIKALI YAWATAKA WANANCHI WALIOVAMIA ENEO LA KAMBI WA WAZEE NUNGE KUSITISHA UJENZI

Naibu Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia , Wazee na Watoto Dkt.Hamisi Kigwangalla (kulia)akitembelea jana Makazi ya Wazee walioathirika na ugonjwa wa ukoma yaliyopo kijiji cha Nunge eneo la Kigamboni jijini Dar es Salaam.mwenye shati la batiki Mkuu wa Makazi hayo Moses Gunza.
Naibu Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia , Wazee na Watoto Dkt.Hamisi Kigwangalla akimsikiliza mmoja wa wazee aliyejulikana kwa jina la Salum Ubwabwa wakati alipotembelea jana Makazi ya Wazee walioathirika na ugonjwa wa ukoma yaliyopo kijiji cha Nunge eneo la Kigamboni jijini Dar es Salaam.Mzee huyo ambaye alimpatia historia ya eneo hilo, ambalo sasa limevamiwa na baadhi ya watu.
Naibu Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia , Wazee na Watoto Dkt.Hamisi Kigwangalla akiangalia mazingira ya makazi hayo.
Naibu Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia , Wazee na Watoto Dkt.Hamisi Kigwangalla akielekea moja ya maliwatoni katika Makazi ya Wazee walioathirika na ugonjwa wa ukoma yaliyopo kijiji cha Nunge eneo la Kigamboni jijini Dar es Salaam, wakati alipofanya ziara ya kutembelea makazi hayo jana ili kuangalia mazingira halisi. (Picha na Sungura (Picha na Catherine Sungura-WAMJW)

Na. Magreth Kinabo-Maelezo

Serikali imewataka wananchi waliovamia eneo la kambi ya kuwalea wazee walioathirika na  ugonjwa wa ukoma yaliyopo Nunge Kigamboni, kusitisha mara moja ujenzi wa nyumba zao ama kubomoa wenyewe ndani ya siku 21 kabla hatua ya kubolewa haijachukuliwa.

Agizo hilo limetolewa na Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii wazee na watoto Dkt. Hamisi Kigwangalla, wakati alipowatembelea jana na kukuta idadi kubwa ya nyumba za wananchi mbalimbali zilizojengwa ndani ya ardhi ya makazi hayo ya wazee.

Kufuatia hali hiyo ,Dkt. Kigangwalla amemuagiza Mkuu wa kambi hiyo ya wazee Moses Gunza kutoa notisi ya kusitisha ujenzi na ikiwezekana wananchi hao wabomoe wenyewe nyumba zao kabla Serikali haijafika kuwabomolea.

“Hivi kweli watu wanaona kabisa makaburi haya watu wamezikwa hapa tangu enzi za mjerumani halafu wananunua na kujenga haiwezekani kuchezewa kiasi hiki watu wafike sehemu waiheshimu Serikali na kufuata sheria za nchi,”alisema Dkt. Kigwangalla.

Dkt. Kigwangalla eneo hilo la Nunge limewekwa kwa ajili ya kulea na kuhudumia watu waliokuwa wakiuugua ugonjwa wa ukoma sasa iweje ajitokeze mjukuu wa kati ya wazee hao awauzie watu na ardhi hiyo huku akidai kuwa eneo hilo ni mali yake iliyotokana na urithi wa babu yake jambo ambalo sio kweli.

“Ninatoa siku 21 watu hawa wote waliojenga katika makazi haya ya wazee kusitisha mara moja ujenzi wa nyumba zao au kubomoa na hiyo mtu anayedai eneo hili ni lake akija hapa akatoa maagizo yake mnipe taarifa nitamuweka ndani.,”alisema Dkt. Kigwangalla.

Akipokea akigizo hilo mkuu wa kambi hiyo Moses Gunze alisema wananchi hao walikwisha pewa notisi tangu mwaka jana 2015 na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya kuwataka wananchi waliopo eneo lote la Nunge kusitisha zoezi la kuendelea kujenga nyumba zao agizo ambalo halikutekelezwa kutokana na muingiliano wa kisiasa.

“Hawa watu Mwanasheria Mkuu wa Serikali alishatoa stop order ya kuwataka wasiindelee na ujenzi wowote hapa lakini baadaye wananchi hawa wakajipanga wakaenda Bungeni Dodoma na baadaye aliyekuwa Waziri wa afya Dkt. Seif Rashid akatoa barua akasimamisha zuio matokeo yake watu wakaendelea kujenga tena, ’’alisema Moses.

Kwa upande wake mzee Salumu Ubwabwa ambayea ameathirika na ukoma anayelelewa katika kituo hicho amebainisha kuwa kuna anayejulikana kwa jina la Bahari Seifu anayewauzia watu viwanja akidai kuwa eneo hilo la Nunge ni lake amerithi kutoka kwa babu yake Mohamedi Sheweji.

Mzee Ubwabwa amebainisha kuwa yeye amefika katika makambi hayo tangu mwaka 1984 baada ya kuugua ukoma kutokana na miaka hiyo watu wa ukoma kutengwa mjerumani akawajengea jumba la mabati na kuwahifadhi huko Kigamboni ili wasiweze kuvuka kwenda ng’ambo kwani wangeweza kusababisha maambukizi.

Alisema mwaka 1974 Rais wa kwanza Hayati Julius Nyerere aliwajengea nyumba hizo na Serikali ya Tanzania ikaendelea kuwatunza hadi sasa.

Mzee Ubwabwa alisema katika makambi hayo alikuwepo na mzee Mohamedi Sheweji ambaye naye alikuwa mgonjwa wa ukoma alihifadhiwa kwenye makambi hayo hivyo anashangaa kuona Bahari Seif akijitokeza hivi sasa na kuanza kuuzia watu viwanja kwa madi kuwa ardhi ya Nunge ni uridhi wa babu yake wakati si kweli.

No comments: