Wednesday, May 1, 2013

Taarifa kwa vyombo vya habari toka kwa Mbunge wa Jimbo la Nzega, Dkt Hamisi Kigwangwalla




Bungeni, Dodoma, Mei 1, 2013.

Nawasalimu kwa heshima na taadhima.
Napenda kutumia fursa hii kutoa taarifa kwa wanahabari na umma kwa ujumla kufuatia habari iliyotoka leo mapema asubuhi kwenye gazeti la Sauti ya watu Tanzania Daima, toleo Na.3071 na kuzua mjadala mkubwa na mzito kwenye jamii pamoja na kwenye mitandao ya kijamii kuhusiana na hadhi, heshima na uadilifu wangu kwenye jamii nikiwa kama kiongozi wa umma. Niwape pole wale wote walioguswa na kushughulishwa na jambo hili, haswa familia yangu, ndugu, marafiki na wananchi wa Nzega; ambao siku zote wanaamini sana katika uadilifu wangu na namna ninavyosimamia misingi ya haki, sheria na uzalendo.
Nimesikitishwa sana na habari  hii hususan kwa kuwa ilichapishwa bila kunipa fursa ya kueleza kwa mapana uhusika wangu. Niwapongeze gazeti la Nipashe kwa kupuuza uzushi huu mara baada ya kunipigia na kueleza upande wangu wa hadithi.
Kumekuwa na wimbi kubwa la baadhi ya watu kwenye baadhi ya vyombo vya habari kuandika habari za uongo kwa maslahi maovu ya kuwachafua wanasiasa na watu wengine. Watanzania sote tubadilike na tukatae tabia za kutumika vibaya namna hii, maana ni hatari kwa ustawi wa weledi, na kwa umoja na mshkamano wa kitaifa. Ukishaandika jambo ambalo litamchafua mwenziyo, hata kama utamsafisha kiasi gani ni wazi hautokuwa na uhakika kuwa utawafikia wale wale waliosoma zile za jana za kumchafua – hivyo ni jambo la kawaida kabisa kuanza kwanza kwa kuwa na uhakika kabisa na habari kabla ya kuiandika.
Mfano mwaka 2010 tu mara baada ya kuteuliwa nilizushiwa kashfa ya uongo kabisa inayohusiana na Uraia wangu na gazeti moja maarufu la kila siku na mengine yakaweka kwenye ukurasa wa mbele kabisa kwamba Kigwangalla ni Mrundi; hawakusema ni mrundi wa wapi, toka lini ama kivipi, walisema ni mrundi tu! Basi hata kusema shaka yao inaanzia wapi hawakusema. Kwa kuwa vyombo vya dola vilinisafisha na kupelekea kushinda mapingamizi yote yaliyowekwa na washindani wangu kisiasa, niliamua kudharau na kusema yatapita tu na yatasahaulika.
Pia gazeti lingine likaandika kwamba kampuni ya Kigwangalla ni miongoni mwa makampuni yaliyowahi kufaidika na ‘stimulus package’ baada ya mdororo wa uchumi mwaka 2008. Gazeti hata halikutaja kampuni ya Kigwangalla ni ipi, inaitwaje, Kigwangalla ana hisa kiasi gani, anaendesha kampuni hiyo ama la, na kampuni hiyo imepewa sh ngapi kutoka benki kuu, na je imepewa pesa hizo kwa nyaraka zipi na zenye namba gani? Na je pesa hizo imepewa kihalali ama imepitia mlango wa nyuma? Kama imezipata pesa hizo kinyume na utaratibu, basi kuna ushahidi gani! Kwa kuwa yalikuwa mambo ya uongo na uzushi niliamua kudharau na kuacha kama ilivyo.
Gazeti lingine la kila siku liliwahi tena kuandika ‘Kigwangalla atajwa kufadhili mgomo wa madaktari’ na liliweka hadithi hii kwenye ukurasa wake wa mbele kabisa. Halikusema amefadhili sh ngapi? Amempa nani? Zimeenda kufanya nini fedha hizo? Kwa kuwa lilikuwa ni jambo la uongo, pia nilidharau na kuacha lipite. Mwaka jana Novemba pia gazeti lingine liliandika habari na kuweka picha yangu na ya Ndg. Hussein Bashe, na katikati yetu picha ya bastola, na kusema ‘Kigwangalla na Bashe na vita ya bastola Nzega’, na humo ndani kueleza kuwa Kigwangalla na Bashe wanyoosheana bastola wakati wakirudisha fomu za kugombea ujumbe wa NEC. Na kuna mengine mengi: yale ya rushwa ya vitumbua n.k.
Yote haya kwa ujumla wake yalikuwa ni mambo ya uongo na yasiyo na chembe ya ukweli hata kidogo. Mara zote nimekuwa nikiyadharau na kuongea na wahariri wa vyombo husika vya habari kwa namna inayoashiria urafiki na weledi wa kushirikiana na kufanya kazi pamoja na si vinginevyo; ushauri ambao niliupata mwaka 2009 kutoka kwa moja ya wanasheria wa kampuni yangu (wa kampuni ya Marando, Mnyele & Co. Advocates), wakili nguli Mzee Mabere Nyaucho Marando, ambaye alisema ‘wasamehe tu hawa gazeti la Sauti Huru maana ni vema kujenga marafiki wengi zaidi na media kwa kuwa wewe ni kijana, kuliko kujenga maadui – na niliwasamehe bila gharama yoyote ile’. Mzee Marando hakukosea, ila ukweli ni kwamba ukifanya hivyo utaona patatulia kwa muda na baada ya hapo pataibuka tena jambo lingine la ukurasa wa mbele linaloandikwa bila ukweli wowote ule! Imekuwa wimbo wa kawaida kwenye baadhi ya media houses! Kufanya kazi kwa maslahi ya watu fulani ama chama fulani, misingi ya weledi ya uandishi haipo! Cha muhimu ni maelekezo ama utashi wa anayetoa chochote. 
Jambo moja kubwa nililojifunza kutokana na yote haya ni kwamba, jambo likiishaandikwa kwenye media halifutiki kwenye bongo za watu, hata muda ukipita namna gani! Leo hii kila siku haya mambo yamekuwa yakirudiwa rudiwa kwenye mitandao ya kijamii hata baada ya kuyatolea ufafanuzi wa kina. Nimefika mahali nimeona niachane na passive ways za kushughulika na media ili kuweka sawa kumbukumbu zangu mbele ya umma wa watanzania.
Ya ukweli: ni kweli kwamba ninamiliki hisa kwenye kampuni ya Emergent Africa Ltd. Nina hisa 40% na mke wangu Dr. Bayoum Kigwangalla anamiliki hisa 11%. Sijihusishi na kuendesha biashara hii kama mtendaji wa kila siku – kampuni ina watumishi wake sehemu mbalimbali. Ni kweli kwamba kampuni ina mradi wa kujenga chuo cha afya Nzega (International Institute for Health Tabora), eneo la uchama, na ni kweli imepewa orodha ndefu ya vitu ilivyosamehewa kodi na serikali kwa kuwa ni vitu/vifaa vya mtaji (deemed capital goods). Ni kweli kwamba kampuni imewahi kuingiza nchini kontena moja lenye vifaa vichache sana katika vinavyotajwa kwenye habari ile, na vingi kati ya hivyo vipo aidha kwenye stoo ya kampuni iliyopo Nzega ama ya Dar es salaam, Kigamboni. Kwa kuwa vipo, wanahabari wanakaribishwa kwenda kuvitazama vitu hivi kama wanapenda.
Ya uongo: Si kweli kwamba nina hisa 78% na mke wangu Dr. Bayoum Kigwangalla ana hisa 22% - ni uongo. Si kweli kwamba kampuni imeagiza vitu na kuvipitisha bandarini na forodhani kwa msamaha kwa nia ya kuuza na hivyo kuiibia serikali kwa njia ya kukwepa kodi. Si kweli kwamba kampuni ya Emergent Africa Ltd imeingiza vifaa vyote ambavyo imepewa msamaha, kama habari inavyotaka kuwaaminisha waTanzania. Sijawahi kuuza bidhaa zozote zile za kampuni hii zilizoingizwa nchini kwa njia ya msamaha wa kodi. Kampuni ya Emergent Africa Ltd haina mradi wa kuuza tiles na hivyo haijawahi kufanya biashara hiyo.  
Ingekuwa ni dhambi kubwa kama kweli ningekuwa naviuza vifaa hivi bila kuvilipia kodi. Na kama ningekuwa sina mradi genuine wa ujenzi wa chuo na labda nimetumia vibaya nafasi yangu ya ubunge kujipatia msamaha ili kurahisisha biashara zangu basi ningeanza kwa kuuza cement (ambayo ni bidhaa inayokimbia sana sokoni na kampuni yangu imepewa msamaha wa karibu tani 5000 – lakini sijawahi kuutumia msamaha huu kununua hata mfuko mmoja wa cement!). Ama ningeingiza mabati/vigae vya kuezekea (ambavyo pia vinakimbia sana sokoni kwa kuwa watu wengi wanajenga – lakini sijaingiza hata kigae kimoja!), ama ningeingiza malori 4, Nissan Navara pick up 4, Mitsubishi Canter 2, Landcruiser Hardtop 4( ambazo zinatumika sana kwenye utalii na hata kwenye barabara za vumbi) kwa msamaha – lakini sijaingiza hata gari moja kati ya haya, kinyume na habari hii ya Tanzania Daima inavyotaka kuuaminisha umma! Kuonesha uadilifu nitaeleza hapa mfano mmoja kwamba mnamo Novemba mwaka jana nilinunua gari moja SUV aina ya Nissan Patrol (T934 CDB) na nimeilipia kodi zote bila msamaha japokuwa ningeweza kutumia msamaha wa kodi kununua na kuingiza moja ya magari yaliyopo kwenye msamaha huu wa kampuni ambayo mimi ni major shareholder. Pia nina ujenzi wa nyumba ya kuishi Nzega, Tabora na Dar es salaam katika hatua mbalimbali: ningeweza kutumia msamaha huu wa kodi wa kampuni yangu ili kujipatia unafuu kwenye manunuzi ya vifaa mbalimbali vya ujenzi kama cement, vigae ama mabati, lakini sijawahi kufanya hivyo hata siku moja!
Kuwa na hisa kwenye kampuni inayofanya biashara halali siyo dhambi. Kupata msamaha wa kodi siyo dhambi. Dhambi ingekuwa kuviuza baada ya kupata msamaha. Kama kuna mtu anaamini kuwa kuna vifaa vimeuzwa na kampuni yangu, kati ya hivi vilivyoingizwa nchini kwa msamaha, anakaribishwa kuleta uthibitisho wa nyaraka za mauzo (cash sale receipts, tax invoice ya mauzo, pay-in slip ya benki ya malipo, delivery note, ama receipt yoyote ile ya kampuni hii inayoashiria kuwa mauzo yamefanyika) ili niweze kufuatilia kujua ni nani aliyeuza na kwa nini alifanya hivyo ili niweze kuchukua hatua za kinidhamu dhidi yake ikiwa ni pamoja na kumpeleka mbele ya vyombo vya sheria.
Msamaha wa vifaa hivi ni kwa ajili ya Ujenzi wa Chuo Cha Afya Nzega (kitakachoitwa International Institute for Health Tabora), ambacho nilikianza kwa fedha zangu mpaka pale kilipofikia na sasa tunasubiria majibu ya benki ya maombi yetu ya mkopo ndipo tuendelee. Na msamaha huo upo na hautotumika kwa mambo mengine ya binafsi kama nilivyoeleza hapo juu kwenye ununuzi wa gari langu binafsi la kutembelea na ujenzi wa nyumba yangu binafsi ya kuishi Nzega, Tabora ama Dar es salaam (ambako ninajenga).
Watanzania tuache kushabikia uongo. Kufanya hivyo kunaziba mianya ya ukweli kutamalaki. Tuache kutazama mambo kwa macho ya wivu, husda na majungu. Tusimame kwenye misingi ya ukweli daima. Nchi hii itaendelezwa na watu wenye kuchukua maamuzi thabiti na hatua za maksudi za kuleta mabadiliko – kama miradi ya namna hii (ya chuo cha afya Nzega kule!). Nchi yetu bado ina watu waaminifu na waadilifu na tunaamini tutafanikiwa kuwadhibiti walio waovu. Hata siku moja kweli haijawahi kushindwa vita na uongo. Si kila mtu aliyeko kwenye uongozi ndani ya CCM basi ni fisadi, watu wazuri na wasafi wapo pia. Tusimuangalie kila mtu kwa sura ya ‘ufisadi’ na ‘ubadhirifu’ tu! Tuaminiane jamani. Tusifedheheshane na kukatishana tamaa. Safari kuelekea mapinduzi ya maisha ya watanzania kiuchumi na kijamii bado ni ndefu lakini tutafika. Tufanyeni kazi.
Taarifa hii nimeiandika na kuitoa mimi mwenyewe, Hamisi Andrea Kigwangalla, M.D., Mbunge, Jimbo la Nzega. (simu yangu ya kiganjani ni 0782636963 na email yangu ni hkigwangalla@gmail.com, website: www.hamisikigwangalla.com )   

No comments: